HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 17, 2017

Naibu Waziri Shonza ahidi kusimamia maadili ya Mtanzania

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza akikabidhiwa ofisi na aliyekuwa Naibu Waziri wizara hiyo Mhe. Anastazia Wambura leo mjini Dodoma.
  
Na Eleuteri Mangi, WHUSM, Dodoma

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza ameahidi kushirikiana na Watendaji wa Wizara, wadau pamoja na wananchi kwa ujumla kusimamia maadili ya Mtanzania ili kuendelea kuwa na taifa bora.

Mhe. Shonza ameyasema hayo alipowasili katika ofisi za Wizara leo mjini Dodoma ambapo alipokelewa na Waziri mwenye dhamana Dkt. Harrison Mwakyembe, viongozi wa Wizara pamoja na  watumishi.

“Wizara hii ni muhimu sana kwa kuwa inajenga taswira ya taifa kupitia sekta zake ambazo ni Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo hivyo ntahakikisha tunashirikiana kwa karibu katika kuwatumikia wananchi “alisema Naibu Waziri Shonza.

Aliongeza kwa kueleza kuwa atahakikisha suala la maadili bora kwa jamii  linazingatiwa ili kuendelea kujenga taifa imara kwa kuzingatia mavazi yenye heshima na  nyimbo zenye kujenga.

Aidha, Naibu Waziri Shonza amesema ni wajibu wetu kama watumishi wa umma kuhakikisha tunatekeleza Ilani ya chama tawala ambacho kiliahidi kuwatumikia watanzania ili kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa kwa wakati.

Naye aliyekuwa Naibu Waziri wa Wizara hiyo Anastazia Wambura amempongeza Naibu Waziri Shonza kwa kuteuliwa kushika wadhifa huo na amemshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumuamini kuwatumikia Watanzania.

Akizungumzia utendaji kazi, Mhe. Wambura ameufananisha utumishi wa umma na chombo cha usafiri ambapo abiria hushuka kituo mara baada ya kufika na dereva kuendelea na safari.

“Mhe.Waziri, viongozi wenzangu na ndugu zangu watumishi wa Wizara, mimi nimefika kituoni, Naibu Waziri nakukabidhi kijiti endelea na safari, endelea kuwatumikia Watanzania kama ambavyo ilani ya chama tawala inavyoeleza” alisema Mhe.Wambura

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe amemuahidi Naibu Waziri Shonza ushirikiano wa hali na mali katika kuwahudumia wananchi kupitia sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

No comments:

Post a Comment

Pages