HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 06, 2017

MADAKTARI 15 WA ZANZIBAR KUPATA MAFUNZO CUBA

Balozi wa Cuba Nchini Tanzania Profesa Lucas Dmingo Herndez aliyesimama akizungumza  katika Mkutano Maalum wa kuwaaga Madaktari Wazalendo wanoelekea Nchini Cuba kwa Mafunzo zaidi ya Udaktari Bingwa hapo katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Vuga Mjini Zanzibar.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Cuba katika kuiunga Mkono Zanzibar  kwenye Miradi ya Maendeleo hasa katika Sekta ya Afya imeanza kuleta mafanikio makubwa ya matumaini.

Alisema kitendo cha Cuba cha kukubali kuwagharamia Kimasomo Madaktari Wazalendo wa Zanzibar  kufikia Utaalamu wa kuwa Madaktari Mabingwa  ni mfano halisi wa matumaini hayo.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo mbele ya Balozi wa Cuba Nchini Tanzania Profesa Lucas Domingo Hernadez Polledo katika Mkutano Maalum wa kuwaaga Madaktari Wazalendo 15 ambao Wanane kati yao  wataondoka wakati wowote kuanzia sasa kuelekea nchini Cuba kwa Mafunzo zaidi ya Udaktari Bingwa.

Madaktari hao Wazalendo wa Zanzibar waliomaliza mafunzo yao kupitia mpango wa masomo ulioasisiwa kati ya Serikali ya Cuba na Zanzibar ni pamoja na Anas Mbarak Anas, Nihifadhi Issa Kassim, Rukia Abdulrahman Sadiq, Salama Makame Pandu, Said Simai Msalaka, Abdullah Omar Khamis, Yassin Khamis Moh’d na Mwadini Maalim Simai.

Balozi Seif alisema kundi la Pili laMadaktari hao  Saba Wazalendo linatarajiwa kwenda Nchini Cuba Mwakani na kukamilisha Idadi ya Madaktari hao 15 kupitia uamuzi wa Cuba wa kukubali kusaidia Sekta hiyo kufuatia ziara ya hivi karibuni aliyoifanya Nchini Cuba kwa kukutana na Uongozi wa Wizara ya Afya pamoja na ile ya Mambo ya Nchi za Nje.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliendelea kuishukuru na kuipongeza Serikali ya Jamuhuri ya Cuba kwa namna inavyoendelea kuunga mkono jitihada za Serikali zote mbili ile ya Zanzibar na ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania  kwa kuwaletea maendeleo Wananchi wake.

Mapema Balozi wa Cuba Nchini Tanzania Profesa Lucas Domingo Hernadez Polledo alisema uhusiano wa kidoplomasia kati ya Cuba na Zanzibar ni wa Kihistoria kiasi kwamba, kupitia muingiliano wa mahusiano ya kubadilishana taaluma utaendelea kuimarika zaidi.

Balozi Lucas aliwakumbusha Madaktari hao wa Zanzibar  kwamba  Wananchi walio wengi wana matarajio ya kupata huduma za Afya zilizo makini kupitia Wataalamu wanaosomeshwa na Serikali kwa lengo la baadaye la kusaidia Jamii inayowazunguuka.

Alielezea matarajio yake kuiona  Zanzibar  ikijiwekea tayari kwa kuwekeza katika miundombinu ya Miradi  mbali mbali  ikiwemo sekta  muhimu ya Afya ili kuleta matarajio kwa Wananchi pamoja na wageni wanaojipangia kutembelea Visiwa vya Zanzibar.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Wizara ya Afya Zanzibar Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bibi Halima Maulidi Salum aliahidi kwamba Wizara ya Afya itaendelea kuwa karibu na Wahadhiri pamoja na Madaktari  Bingwa kutoka Nchini Cuba wanaotoa mafunzo kwa Madaktari Wazalendo Visiwani  Zanzibar.

Bibi Halima alisema nafasi zozote za kimasomo zitakazopatikana za kuongeza Taaluma kwa Madaktari na Watendaji wao, Wizara itajitahidi zaidi kuzichangamkia ili kuwajengea uwezo watendaji na Madaktari hao.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
4/11/2017.

No comments:

Post a Comment

Pages