HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 16, 2018

Rais Magufuli Mgeni Rasmi Mkutano wa Baraza la Mawaziri Bonde la Mto Nile

Jonas Kamaleki, MAELEZO, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuri atakuwa Mgeni Rasmi katika Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri wa Nchi za Bonde la Mto Nile zilizopo kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dodoma, Waziri wa Maji, Prof. Makae Mbarawa amesema Mkutano huo utapitia utekelezaji masuala mbali mbali ya miradi, utapokea taarifa ya utendaji, hali ya ulipaji wa michango ya kila mwaka kwa nchi wananchama na tathmini ya watumishi wa Sekretarieti ya NELSAP.

Mkutano huo ambao utafanyika Jijini Dar es Salaam Novemba 22, 2018 utawashirikisha mawaziri wa Maji na wawakilishi kuto nchi za Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Misri, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Sudan, Sudani ya Kusini na Uganda.

Prof. Mbarawa amesema kuwa Mkutano huu utatanguliwa na vikao vya wataalamu ambavyo ni vya kiutendaji na vitaanza tarehe 20 hadi 21 Novemba, 2018 Jijini Dar es Salaam.

“Ushirikiano wa Nchi za Bonde la Mto Nile ni wa muda mrefu, umeanza tangu miaka ya 1960 na ilipofika tarehe 22 Februari, 1999 nchi wanachama ziliunda Taasisi ya Mpito ya Bonde la Mto Nile iitwayo Nile Basin Initiative-NBI. Taasisi hii ilianzishwa Dar es Salaam, na sasa inaelekea kutimiza miaka 20,”alisema Prof. Mbarawa.

Bonde la Mto Nile ni ukanda wote wa eneo la Bonde la Mto huo kuanzia Ziwa Victoria hadi Bahari ya Mediterania ambapo Tanzania iko sehemu ya juu ya Bonde la Mto Nile ambako Mto Mara, Simiyu na Mto Kagera inamwaga maji katika Ziwa Victoria ni sehemu ya Bonde hilo. Mto Nile ni mrefu sana Duniani kwa kuwa na urefu wa kilomita 6,695.
 
Tanzania ni miongoni mwa nchi 10 za Bonde la Mto Nile zinazoshirikiana katika kusimamia na kuendeleza Raslimali za Maji za Bonde la Mto huo chini ya mwavuli wa NBI.

No comments:

Post a Comment

Pages