HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 21, 2019

Waratibu Tamasha la Pasaka wahaha kutafuta uwanja Dar

 Mkurugenzi wa Kampuni ya Msama Promotions, Alex Msama, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kuhusu maandalizi ya tamasha la Pasaka. Kushoto ni Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya tamasha hilo, Saleh Mohamed. (Picha na Francis Dande).



    NA MWANDISHI WETU

    WAKATI maandalizi ya Tamasha la Pasaka yakizidi kushika kasi, shauku kubwa ya wadau wa muziki wa injili, ni kujua vichwa gani vitapamba tukio hilo la kimataifa litakalozinduliwa jijini Dar es Salaam April 21 kabla ya kuhamia mikoani.

    Pamoja na shauku hiyo kwa wapenzi wa mashabiki wa muziki wa injili kote nchini, kwa wale wa jijini Dar es Salaam, kumekuwa na mabadiliko ya uwanja wa kufanyia tukio hilo la aina yake litakalowaleta pamoja waimbaji wa kitaifa na kimataifa. 

    Ingawa awali, Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hili ilitangaza kwamba uwanja wa TTCL Kijitonyana uliopo wilayani Kinondoni ndio ungetumika kwa kishindo cha tukio hilo kwa jijini Dar es Salaam, lakini umekosekana kwa siku hiyo.

    Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hilo, Alex Msama alisema ni kweli walipenda sana tukio hilo lifanyike hapo, lakini wamiliki wake wamesema kwa siku hiyo ya April 21, haitawezekana.

    “Kweli tulipenda sana Tamasha la mwaka huu, lingefanyika katika Uwanja wa TCCL Kijitonyama kutokana na kufikia vigezo tulivyotaka, lakini sasa tumeukosa kwa sababu wenyewe wamesema siku hiyo kutakuwa na shughuli nyingine,” alisema Msama.

    Akionyesha kusikitishwa na hali hiyo, Msama alisema kwa sasa kamati yake inaendelea kutafuta eneo jingine ambalo watafanyia tukio hilo na kudokeza  tayari wanayafikiria maeneo mawili ambapo wanaendelea na mazungumzo.

    Msama alisema, pamoja na kujitokeza kwa hali hiyo, azma ya kufanya tamasha hilo jijini Dar es Salaam, bado ipo hasa kutokana na wadau wa jiji hilo kuukosa uhondo wa tamasha hilo kwa miaka mitatu.

    “Wadau wetu wa muziki wa injili wa jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake, wameikosa uhondo wa Tamasha la Pasaka kwa miaka mitatu kutokana na kufanyika mikoani pekee, hivyo tusingependa walikose kwa mara nyingine,” alisema Msama.

    Kuhusu waimbaji, Msama alisema mazungumzo na waimbaji yapo katika hatua za mwisho na kuanzia wiki ijayo, wapenzi na wadau wa muziki wa injili wataanza kuwajua watakaobeba tamasha hilo. 

    Msama alidokeza kuwa, kigezo kikubwa kilichotumiwa katika uteuzi wa waimbaji hao, kwanza ni uwezo wa kuimba ‘live’ jukwaani kwa maana pasipo kutumia ‘CD’ hasa kwa wale wazawa ili kuwajengea uwezo na ujasiri wawapo jukwaani.

    “Unajua, kitendo cha mwimbaji kuimba nyuma ya CD, kunawalemaza, unaweza kumuona mwimbaji ni mzuri sana jumwaani, lakini kumbe ni kutokana na staili hiyo, lakini pale anapoimba ‘live’, huwa ni mwingine kabisa,” alisema Msama.

    Msama alisema kuwa, ingawa mfumo huo unaweza usiwe rafiki sana kwa baadhi ya waimbaji kuona kama wanakomolewa, lakini unawajengea uwezo na hali ya kujiamini kuimba ‘live’ jukwaani hata wanapoalikwa kwenda nje ya Tanzania.

    Kwa upande wa malengo, Msama alisema kuwa mbali ya malengo ya msingi ambayo ni kueneza Neno la Mungu na kutumia sehemu ya mapato kufariji makundi maalumu, safari hii tukio hilo litabeba ajenda nyingine mahsusi.
    Msama alizitaja ajenda hizo ni kuhimiza amani na umoja wa kitaifa kwa kutambua kuwa huo ndio msingi wa maendeleo, kwa upande wa kijamii, kiuchumi pamoja na kisiasa.

    “Mbali ya maudhui ya jumla, mwaka huu tutakuwa na ajenda nyingine za ziada kama kuhimiza amani hasa kwa kuzingatia kuwa, nchi itaingia katika chaguzi za serikali za Mtaa, hivyo hali ya amani inapaswa kutamalaki,”  alisema Msama.

No comments:

Post a Comment

Pages