HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 10, 2019

NMB ‘kusomesha’ wafanyabiashara 10 China

Mchoraji kutoka Tingatinga Arts, Agnes Mpate alkimuonyesha picha ya kuchora Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB Albert Jonkergouw wakati wa Kongamano la wafanyabiashara Business Club Ilala lililofanyika leo  jijini Dar es Salaa.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB Albert Jonkergouw akiangalia moja ya bidhaa za Mkurugenzi wa Malaika Home essentials, Rachael Moyo wakati wa Kongamano la wafanyabiashara Business Club Ilala lililofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha biashara, Donatus Richard.


NA MWANDISHI WETU

KATIKA kuwaongeza uelewa, maarifa na elimu ya kujenga nidhamu ya fedha kwenye biashara zao, Benki ya NMB imeahidi kuwapeleka China kwa masomo na warsha wafanyabiashara 10 kutoka katika Klabu za Biashara za benki hiyo ‘NMB Business Club,’ baadaye  mwaka huu.

Ahadi hiyo imetolewa jana jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa NMB, Donatus Richard, wakati wa kongamano la Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati (MSE), wanaounda Klabu za Biashara za NMB, iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kardinali Rugambwa, Oysterbay.

Richard alibainisha kuwa, lengo la ziara hiyo ya mafunzo ni kuimarisha uelewa wa masuala ya fedha miongoni mwa wafanyabiashara wanaounda klabu hizo, lengo likiwa ni kuwaongezea elimu ya kuhakikisha mtiririko wa fedha kwenye biashara zao, unakuwa mnyoofu.

Akisisitiza ahadi hiyo, mbele ya wafanyabiashara zaidi ya 300 walioshiriki kongamano hilo, Richard alisema kuwa mchakato wa namna ya kuwapata wateule wa ziara hiyo utatangazwa miongoni mwao,ili kwenda kupata fursa za kimataifa, safari ikitarajiwa kufanywa Oktoba mwaka huu.

“Ushindani kibiashara nchini umekuwa mkubwa, nasi ndio maana tunatumia klabu hizi kufundisha mifumo, njia na mipango rafiki ya kuimarisha biashara za wateja wetu hawa ambao pia ni mabalozi wetu kwa jamii. Tutawapeleka China kujiongezea maarifa juu ya hilo,” alisema Richard.

Awali akifungua kongamano hilo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Albert Jonkergouw, alisema watayafanyia kazi mapendekezo yote yatakayotolewa na wafanyabiashara wanaohudhuria makongamano yao kutoka klabu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na punguzo la gharama za uendeshaji wa akaunti ya biashara.

Jonkergouw alibainisha ya kwamba, Klabu za Wafanyabiashara ni nzuri na muhimu sio tu kwa wanachama wake na Benki ya NMB, bali pia kwa ustawi na ukuaji wa uchumi wa Taifa na kwamba wafanyabiashara hao ni kati ya mabalozi wema wa benki hiyo.

“Kongamano hili ni kati ya fursa tunazozitumia kusikiliza changamoto zenu, kujadiliana namna ya kuzitatua na mwisho wa mwezi kwenda pamoja katika kasi ya uchumi wa mteja mmoja mmoja, benki kama taasisi na taifa kwa ujumla wake,” alisisitiza Jonkergouw.

Akizungumza kwa niaba ya wafanyabiashara waliohudhuria, aliishukuru NMB kwa kuwakabidhi baadhi yao vyeti vya ubalozi mwema wa benki kwa wafanyabiashara wa kupigiwa mfano, Award Mpandila, aliitaka Serikali kuwasaidia ujenga mazingira rafiki ya kibiashara.

Mpandila alifafanua kwamba, moja ya changamoto zinazokwaza biashara zao ni tozo zisizo wazi hususani bandarini, ambazo zinawakwamisha na kusababisha kutorejesha mikopo yao kwa wakati, kutokana na kuchelewesha kwa uondoshaji mizigo bandarini.

No comments:

Post a Comment

Pages