HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 11, 2019

WAZIRI MKUU ASISISTIZA UMUHIMU WA KUWA NA MITAALA INAYOKWENDA NA MABADILIKO ILI KUWEZA KUZALISHA WANATAALUMA WATAKAO LETA MAENDELEO NCHINI

Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mhe. Stephen Wasira akimkaribisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati alipowasili katika Chuo hicho kufungua Kongamano la Kumbukizi ya Mwalimu Nyerere.


 
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx 


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ameutaka uongozi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili  kuona namna bora ya kuhuwisha  mitaala ya Chuo hicho ili kifikie viwango vya Elimu ya Juu. 


Mhe. Majaliwa ametoa kauli hiyo Jijini Dar es Salaam wakati akifungua kongamano la maadhimisho ya Kumbukizi ya Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambapo amesema  mpaka sasa Chuo hicho kimekidhi viwango vya kuwa na hadhi ya Chuo Kikuu na kwamba elimu inayotolewa katika chuo hicho ndio inasisitizwa nchini.

Ameutaka uongozi wa chuo hicho kutia mkazo katika mafunzo ya uongozi na maadili hususan yale yenye mwelekeo wa kujenga uzalendo na kuendelea kutumia fursa ya uwepo wa makongamano kukuza uelewa wa jamii ya watanzania kuhusu umuhimu wa kuenzi falsafa za mwalimu katika umoja, upendo, uzalendo, uadilifu na mshikamano wa kitaifa.

Aidha Mhe. Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwa kujenga misingi ya Amani, umoja na kuleta maendeleo ya jamii nchini kwa vitendo na kuwataka watanzania kuzingatia maadili, uzalendo na utaifa katika uwajibikaji  wa kila siku, kuungana kwa pamoja bila kujali itikadi za kisiasa au kabila katika kulinda na kudumisha tunu hizo.
“Nimpongeze Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi anazochukua ili kuhakikisha anairejesha nchi yetu kwenye misingi yake ya awali ambayo ni kuwa na viongozi waadilifu, wazalendo na wenye kulinda Amani na kudumisha umoja katika jamii, watanzania wote tunapaswa kuunga mkono jitihada hizi na kuzilinda kwa nguvu zote,” alisema Mhe. Majaliwa.

Naye Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema ni vizuri kumuenzi Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kuwa ni mtu ambaye amelipigania Taifa na kuliletea ukombozi na kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kufuata nyayo za Baba wa Taifa.

Waziri Ndalichako ameeleza kufurahishwa na ushiriki wa wanafunzi katika kongamano hilo kwa kuwa linawapa fursa ya kupata uelewa mpana wa zaidi ya kile wanachofundishwa shuleni, na kwamba taifa linawategema kuwa chachu ya mabadiliko katika nchi.

Awali Mwenyekiti wa Bodi ya uendeshaji wa Chuo cha Kumbu Kumbu ya Mwalimu Nyerere Steven Wassira alimweleza Waziri Mkuu kuwa wanaomba katika kumenzi Baba wa Taifa Chuo hicho kipandishwe hadhi na kuwa Chuo Kikuu na kwamba mazingira yake yaboreshwe yawe na hadhi ya Hayati Baba wa Taifa.

Kwa upande wake mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Prof. Shadrack Mwakalila amesema, uongozi wa chuo hicho unaendelea na maboresho ya kutoa taaluma yenye kujenga uzalendo kwa vijana wa kitanzania.
Kongamano la Maadhimisho ya Kumbukizi ya Baba wa Taifa limechagizwa na mada isemayo Mchango wa Mwalimu Nyerere katika kujenga Amani, umoja na Kuleta Maendeleo ya Jamii nchini. 

Imetolewa na
Kitengo cha Uhusiano
Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.
11/04/2019

No comments:

Post a Comment

Pages