HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 25, 2019

Makabwela  wasifu wazo la kuandaliwa bima wanazozimudu


Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

 
WAZO la kuwaandalia aina za bima watakazozimudu wananchi wenye pato dogo limesifiwa na baadhi ya makabwela ambao wamehojiwa jana. 
 
Wazo hilo limetolewa na Kamishna wa Bima nchini, Dk. Baghayo Saqware, ambaye hivi majuzi amechaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Wasimamizi wa Kampuni za Bima Afrika (AAISA) katika mkutano wa mkuu wa pili wa
 AAISA. 
 
Dk. Saqware amesema kuna haja ya kujenga utamaduni wa wananchi wenye pato dogo kuwa na bima za aina mbali mbali wanazozimu kwa sababu bima ni muhimu kwa mtu yeyote.
 

Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Bukoba kuhusu wazo hilo, kiongozi wa umoja wa wakulima unaojulikana kama WAKUVI amekaribisha wazo hilo lakini akasema wakulima wengi wa daraja lake wana elimu kidogo juu ya bima na watasita kujiingiza katika makubalino ya kampuni za bima kwa sababu hawawezi kumudu malipo ya mara kwa mara kwa kampuni hizo.
“Tunahitaji elimu juu ya mambo haya ya bima na faida zake kwa sababu hatutaki kupoteza fedha kidogo tunayopata. 
 
 Sisi tunalima mazao na kilimo ni biashara ya kubahatisha. Kahawa, vanilla na viazi tunavyolima ni mazao yasiyotupa pato wakati wote kutuwezesha kulipia bima. Pato letu ni kidogo na ni la msimu,” amesema. Hata hivyo amekiri kuwa bima ya afya imeibua na kuonyesha umuhimu bima katika jamii.

Kikundi cha WAKUVI kimesajiliwa na Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi, Mkoa wa Kagera. Mfanyabiashara mdogo wa Jijini Dar es Salaam, Bw Issa Ramadhani Mumba, naye kaona wazo hilo ni chanya lakini kasema pato la makabwela ni dogo kiasi kwamba wanaona haiwezekani kuwa na bima. “Kweli sisi ni watu wa pato la chini, lakini biashara zetu ni biashara za kutupa riziki tu. Tukipata kula yetu tunashukuru. 
 
 Mambo ya bima bwana yako mbali na sisi,” ameeleza. Mtafiti Mkuu katika Mamlaka ya Usimamizi wa Shughuli za Bima (TIRA),
 Dk Emmanuel Lupilya, ambaye amehudhuria mkutano huo pamoja na Dk. Saqware amesema kama nchi kuna haja yakuwa na ubunifu wa maendeleo, ujasiri katika uongozi na mipango ya kimkakati itakayoleta mabadiliko na ubora zaidi katika sekta ya bima.
 
 Mkutano huo wa pili wa AAISA, ambao umefanyika Johannesburg, Afrika ya Kusini, umemchagua tena Bw Boubacar Bah wa Guinea kuwa rais wa umoja huo kwa kipindi kingine cha miaka miwili. Dk. Saqware ni Kamisha wa Bima nchini na Pia Mkurugenzi Mkuu wa TIRA.


No comments:

Post a Comment

Pages