HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 13, 2019

Helkopta, farasi, mbwa, magari kulinda wageni SADC

NA SULEIMAN MSUYA

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limesema kuanzia leo litatumia helkopta, farasi, mbwa na magari kufanya doria ya kuwalinda wajumbe wa Mkutano wa 39 wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Aidha, waendesha bodaboda 87, bajaji 13 na magari 26 wamekamatwa kwa kukaidi maagizo ya jeshi la polisi.

Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi wa Kanda huyo Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.

Alisema kuanzia leo wataanza kutumia helkopta ili kuimarisha ulinzi na usalama kwa wageni na raia wote wa jiji.

Kamanda Mambosasa alisema wiki mbili zilizopita wamekuwa wakifanya doria kwa kutumia mbwa, farasi na magari ambapo usalama upo kila kona.

Mambosasa alisema katika kuhakikisha usalama unaimarika Jeshi la Polisi Kanda Maaalum limeongezewa zaidi ya askari 300 kutoka naeneo mbalimbali.

Alisema jeshi hilo limejipanga kikamilifu kukabiliana na uhalifu na kuwataka watu wenye mpango huo kuacha kwani hawatakuwa salama.

"Leo tunaanza kutumia helkopta kufanya doria ya kukabiliana na uhalifu, nasisitiza hatukuwa na huruma na mtu yoyote anayevunja sheria kwani tunataka wageni wetu wa SADC wafurahie mkutano," alisema.

Alisema askari wamesambazwa kila kona ya jijini hivyo asitokee mtu kuvunja sheria  akihisi yupo salama.

Kuhusiana na watu walikamatwa kwa kuingia mjini kinyume cha sheria, kupiga ving'ora na kutumia taa za mwanga mkali alisema hadi jana wamefikia 126.

Alisema zoezi hilo la kukamata wahalifu hasa boda boda ni endelevu ambapo hadi sasa wamekamtwa 87, bajaji 13 na magari 26.

"Hawa boda boda naona hawajatuelewa kila siku tunawakamata na tutaendelea kuwakamata na hatua za kisheria zitafuata," alisema.

Alisema kundi la bodoboda limekuwa changamoto kubwa kulidhibiti lakini hawatarudi nyuma mkapa wanyooke.

Kamanda Mambosasa alisema operesheni ya kukabiliana na uhalifu itakuwa endelevu na isichukuliwe kuwa ni kwa sababu ya mkutano wa SADC.

Alisema mkutano wa SADC unakutanisha viongozi wakuu wa nchi 16 na wasaidizi wao hivyo unapaswa kuwa na ulinzi wa hali juu.

"Kuna ule msemo wa mtoto mkaidi anafaidi siku ya Eid niwakumbushe kuwa Eid imepita wanaweza wasifaidi kwani tumejipanga vizuri," alisema.

Mkutano wa SADC unashirikisha viongozi wakuu wa nchi za Tanzania, Malawi, Msumbiji, Madagascar, Mauritius, Comoro, Shelisheli, Botswana, Namibia, Angola, Afrika Kusini, DRC Congo, Zambia, Zimbabwe, Eswatini na Lesotho.

Katika mkutano huo ambao unatarajiwa kufanyika Agosti 17 hadi 18 Rais John Magufuli anatarajiwa kupokea kijiti cha Uenyekiti kutoka kwa Rais wa Namibia Hage Geingob anayemaliza muda wake.

No comments:

Post a Comment

Pages