HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 11, 2019

Kubenea awapigania watu wenye Ualbino

 Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana na kuitaka Serikali kuridhia na kusaini Itifaki ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu kuhusu haki za watu wenye ualbino. Kutoka kushoto ni Mwanasheria wa Under the Same Sun, Kondo Seif, Katibu wa Chama cha Watu wenye Ualbino Wilaya ya Ubungo, Mwamvua Kambi, Mwenyekiti wa Chama cha Watu wenye Ualbino Wilaya ya Ubungo, Mussa Geuza na Pendo Manoni. (Picha na Francis Dande).


NA JANETH JOVIN

Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema), ameitaka serikali kuchukua hatua za haraka kuridhia na kusaini Itifaki ya Mkataba wa Afrika wa haki za binadamu kuhusu haki za watu wenye ualbino.

Amesema mkataba huo uliopitishwa mwaka jana katika mkutano wa 30 wa wakuu wa nchi za Umoja wa Afrika haujasainiwa mpaka sasa,  licha ya kwamba unatambua na kuvisemea vitendo vya mauaji na ukatwaji viungo kwa watu wenye ualbino barani Afrika.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Kubenea alisema atapeleka hoja binafsi kuitaka serikali kuridhia na kusaini itifaki ya mkataba huo, kwani watu wenye ualbino nchini ni jamii iliyopo hatarini kufutika kutokana na wengi wao kuuawa kwa imani za kishirikina.

Alisema kwa kuwa itifaki ya mkataba huo imetambua mambo hayo yote hivyo ni muhimu kwa serikali kuridhia na kuisaini haraka, ili ufanye kazi.

“Hata hivyo Itifaki hii pia imezipa majukumu nchi wanachama kuchukua hatua madhubuti za kisera, kisheria, kiuongozi, kitaasisi, na kibajeti, ili kukomesha ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu ingawa Itifaki hii bado haijaridhiwa na kusainiwa na nchi yetu.

“Kuridhia na kusainiwa kwa itifaki ya mkataba huu wa Afrika, sio tu kutaonyesha juhudi na hatua za kimataifa kutangaza dhamira njema ya kudumisha haki na ustawi wa wananchi wenye ualbino na kundi la watu wenye ulemavu kwa ujumla, bali pia kutaifanya nchi yetu kuwa mfano wa kuigwa na jumuiya ya nchi wanachama wa Umoja wa Afrika ambazo pia zinakabiliana na changamoto hii,” alisema.

Hata hivyo Kubenea ameiomba Serikali kufanya marekebisho ya Sera ya Watu wenye ualbino iliyotungwa mwaka 2004 ili ikidhi mahitaji ya makundi yote.

Mwanasheria wa Shirika la Kimataifa la Under the Same Sun, Maduu William, alisema Afrika ndio taifa pekee ambalo watu wake wanaamini, ili wawe matajiri lazima wapate kiungo au nywele ya mtu mwenye ualbino.

Alisema ili kuondokana na dhana hiyo, itifaki hiyo  inapaswa kuridhiwa na kusainiwa, kwani inapinga jambo hilo kwa nguvu zote.

Mwenyekiti wa Chama cha Watu wenye Ualbino Wilaya ya
Ubungo, Mussa Geuza, aliwaomba wabunge wengine waungane na Kubenea kuwatetea na kuhakikisha itifaki ya mkataba huo inaridhiwa na kusainiwa na serikali.

No comments:

Post a Comment

Pages