HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 21, 2019

Tanzania yataja vipaumbele vitatu SADC

NA SULEIMAN MSUYA
NCHI ya Tanzania ambayo ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) imetaja mambo matatu muhimu ambayo itayapa kipaumbele katika kipindi cha mwaka mmoja wa uongozi wake ndani ya jumuiya hiyo.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi wakati anazungumza na waandishi wa habari leo Agosti 21, 2019 jijini Dar es Salaam.
Waziri Kabudi alisema pamoja na mambo mengine wamejipanga kuelekeza mambo muhimu matatu yatakayopewa kipaumbele kwa maslahi ya jumuiya.
Alisema jambo la kwanza ni kuhakikisha lugha ya Kiswahili inazungumzwa kwenye nchi za jumuiya hiyo na hiyo ni baada ya wakuu wa nchi hizo kuipitisha rasmi kuwa lugha ya nne.
Profesa Kabudi alisema haikuwa kazi rahisi kukipigania Kiswahili kuwa lugha rasmi kwenye nchi hizo na kwamba mkakati wake ulianza Machi mwaka huu na kuwataka Watanzania wajipange vizuri kutumia fursa hiyo.

"Mkakati wa kukipigania Kiswahili baada ya majadiliano ya muda mrefu kwenye kikao cha mawaziri wa nchi wanachama wa SADC ,hatimaye Mwenyekiti wa Jumuiya alitoa ombi kwa wakuu wa nchi na hatimaye imepitishwa.
"Ni jukumu letu Watanzania kuhakikisha tunachangamkia fursa hiyo ikiwemo ya kufundisha Kiswahili.Kwa sasa nchi za Kenya na Congo wananufaika sana na lugha hii maana wengi wao wamekuwa walimu wa Kiswahili kwenye mataifa mengine.Nasi tuna kila sababu ya kutumia fursa hii,"alisema.
Waziri Kabudi alisema pamoja na fursa hiyo ya lugha ya Kiswahili kukubalika kutumika katika nchi 16 za SADC pia Watanzania wanapaswa kujifunza lugha nyingine kama Kifaransa na Kireno.
“Ni faraja ambayo haina kifani kwa Kiswahili kukubalika katika ukanda wetu naomba tutumie fursa hii isijekuchukuliwa na watu wengine kwani kwa sasa walimu wengi wa Kiswahili wanatoka Kenya na DRC Congo,”alisema.
Waziri Kabudi alisema jambo la pili ambalo litapewa umuhimu ni kuhakikisha mkakati wa viwanda kwa nchi wanachama unatekelezwa kama ambavyo wamekubaliana wakuu wa nchi hizo.
Alisema ambacho kitafanyika ni kuwepo kwa mpango mkakati kwa kila nchi kufanikisha uwepo wa viwanda kwa maendeo ya nchi hizo.
Aidha, alifafanua matarajio yao ni kuona kunakuwa na kiwanda au viwanda vya mfano kwa nchi za SADC huku akifafanua namna ambavyo Serikali ya Tanzania imejipanga kikamilifu kwenye eneo hilo.
"Tanzania tumepiga hatua sana katika viwanda , na hata kwenye maonesho ya bidhaa kwa nchi za SADC bidhaa zetu zimekuwa kivutio kutokana na ubora wa bidhaa zetu.Waliotembelea viwanda vyetu wamethibitisha na kufurahishwa na teknolojia ya hali ya juu katika utengenezaji bidhaa,"amesema.
Alisema katika kuhakikisha sekta hiyo inakuwa kwa kasi SADC imedhamiria kuondoa vikwazo vya kisera na sheria, kusisitiza ubora wa bidhaa na kuondoa mizani nyingi ili mizigo ifike kwa haraka.
Profesa Kabudi alitaja jambo la tatu kuwa ni kuhakikisha nchi za jumuiya hiyo zinasimama kidete katika kushinikiza jumuiya ya kimataifa kuoindole vikwazo nchi ya Zambabwe.
Alisema na katika kutekeleza hilo wamekubaliana nchi zote za SADC Oktoba 25,2019 iwe ni siku ambayo kutakuwa na shughuli au mijadala kwa kila nchi inayozungumzia Zimbabwe kuondolewa vikwazo vya kiuchumi.
Waziri Kabudi alisema hakuna sababu ya nchi hiyo kuendelea kuwa na kuwekewa vikwazo wakati wananchi wamefanya uchaguzi  na kupata Rais wao kwa uhuru na kusisitiza kuendelea kuiwekea vikwazo nchi hiyo ni kuendelea kuwatesa wananchi.
"Kama kuliwa na sababu za nchi hiyo kuwekewa vikwazo kwa sasa tunaamini havipo tena.Jumuiya ya Kimataifa itoe vikwazo kwa Zimbabwe.Tumekubaliana katika mkutano wa Umoja wa Mataifa mwaka huu tutakwenda na ajenda hii, lazima Zimbabwe iondolewe vikwazo na kuwa Tanzania ndio Mwenyekiti wa SADC tumedhamiria katika hili,"amesema Waziri Kabudi.
Kwa upande mwingine Kabudi alisema Tanzania inaunga mkono ombi la nchi ya Burundi kujiunga SADC na kwamba hadi sasa nchi hiyo imetimiza asilimia 70 ya vigezo vinavyohitajika.
Alisema Burundi imebakiza vigezo viwili ambapo kimoja wapo ni kukubali kutoa ada ya kila mwaka hivyo ikitimiza jumuiya hiyo itaangalia hatua nyingine.
Aidha, Prof. Kabudi amevishukuru vyombo vya habari na waandishi kwa kuonesha uzalendo wa hali ya juu kwenye kuripoti habari za SADC na kuwataka waendelea na utamaduni huo.

No comments:

Post a Comment

Pages