HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 21, 2020

KIFO CHA MCHUNGAJI RWAKATARE CHAWAGUSA WENGI

Mchungaji Getrude Rwakatare

Na Mwandishi Wetu
 
MCHUNGAJI wa Kanisa  la Mlima wa Moto (Mikocheni B) Askofu  Getrude Rwakatare amefariki dunia.
Mchungaji Rwakatare ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), alifariki dunia jana alfajiri katika Hospitali ya Ribininsia   jijini Dar es Salaam wakati akiendelea na matibabu.
Kifo cha askofu Rwakatare  kimewagusa watu wa kada mbalimbali ambao mara baada ya tangazo la kifo chake kila mmoja kwa wakati wake na kwa namna walivyomwelewa kiongozi huyo wa kiroho, walilizwa na kifo chake cha ghafla.
Waliotikiswa zaidi na msiba huo ni waumini wa kanisa lake, wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, walimu, wanafunzi na wazazi ambao watoto wao wanasoma katika shule zake maarufu za St. Marys.
Miongoni mwa walioguswa na kifo cha Mchungaji Rwakatare ni Rais John Magufuli.
Katika salamu zake za rambirambi, Rais Magufuli alielezea kusitushwa na msiba huo na kutuma salam za rambirambi kwa familia, wabunge na waumini wa Kanisa la Mlima wa Moto kufuatia kifo cha Mchungaji Rwakatare.
Katika salamu hizo, Rais Magufuli ameelezea alisema Askofu Rwakatare  alikuwa mcha Mungu, mwenye upendo, asiye na majivuno, aliyepigania umoja na amani na aliyeipenda nchi yake kwa dhati.
Pamoja na kutoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki, Rais Magufuli alimwomba Spika wa Bunge Job Ndugai kufikisha salamu zake za pole kwa wabunge wote na pia amewapa pole waumini wa Kanisa la Mlima wa Moto ambalo Askofu Rwakatare alikuwa kiongozi wake.
“Katika kipindi hiki cha majonzi, tumuombee Askofu Rwakatare apumzike mahali pema peponi, na nawasihi waumini wa Kanisa la Mlima wa Moto muendelee kuwa wamoja na muendeleze mazuri yote yaliyofanywa na Askofu Rwakatare wakati wa uhai wake,” alisema  Rais Magufuli. 
Naye Spika Ndugai, alisema kuwa amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Mchungaji Dk. Rwakatare.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Kimataifa Ofisi ya Bunge, Ndugai alisema anatoa pole kwa wafiwa wote wakiwamo familia ya marehemu, ndugu, jamaa, wabunge na waumini wa Kanisa la Mlima wa Moto (Mikocheni B Assemblies of God).
“Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu,” alisema Spika Ndugai katika taarifa hiyo.
Aidha, Spika Ndugai alisema ofisi ya Bunge kwa kushirikiana na familia ya marehemu inaratibu mipango ya mazishi na taarifa zaidi zitaendelea kutolewa.
 
Akizungumzia kifo hicho, Mchungaji wa kanisa hilo, Stanley Nnko alisema Askofu Rwakatare amefariki dunia baada ya hali yake kubadilika ghafla na kupelekwa katika Hospitali ya Rabininsia iliyopo Tegeta jijini Dar es Salaam.
Alisema mchungaji Rwakatare alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa kisukari na presha na ndio magonjwa yaliyosababisha kifo chake.
“Baada ya afya ya mama kubadilika  alipelekwa hospitalini ambapo alibainika kuwa anasumbuliwa na presha na kisukari, juhudi kubwa  zilifanyika katika kuokoa maisha yake  lakini hazikuzaa matunda,” alisema Nnko.
Nnko alisema hadi sasa bado hawajatoa taratibu za mazishi kwani bado wanaendelea na vikao hadi pale watakapopata taarifa kamili kutoka kwa timu ya madaktari waliokuwa wakimtibu.
"Waumini wa kanisa letu baadhi tumekusanyika kanisani na upande wa familia wapo nyumbani wakiendelea na vikao vya kifamilia, huku tukisubiria mwongozo kutoka kwa daktari ili tujue namna gani tutaweza kumpumzisha mpendwa wetu," alisema Mchungaji Nnko.
Hata hivyo, aliwataka waumini na wananchi wote kuendelea kuwa wavumilivu hadi pale taarifa kamili zitakapopatikana na zaidi waendelee na maombi ya kumuombea Mchungaji Rwakatare, ili apumzike kwa amani.
Mwanae Muta Rwakatare alithibitisha kifo cha mama yake na kwamba alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo ambapo hali ilibadilika na kumkimbiza hospitali.
Mchungaji Rwakatare alizaliwa 31 December 1950,  alisoma Shule ya Msingi Ifakara kuanzia mwaka 1962 na kumaliza elimu ya sekondari 1971   na baadae alisoma chuo kikuu.
1987 aliazisha shughuli mbalimbali za kijamii kama Shule ya msingi na Sekondari za St.Mary katika Mkoa Dar es Salaam, Morogoro, Mbeya, Dodoma na Mwanza Chuo cha Uwalimu cha St.Mary.
Mwaka 1995 aliazisha Kanisa la  Assemblies of God Mikocheni B, ambapo kabla ya hapo alifanya kazi katika Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) jijini Dar es Salaam na alipata PH.D Digrii ya Maendeleo ya Jamiii na Elimu Kristo
Mwaka 2006 aliazisha Kituo cha kulelea watoto yatima ambacho kilikuwa kinafadhiliwa na kanisa lake.
Mwaka 2007 ateuliwa na Rais wa Awamu ya Nne Jakaya Kikwete kuwa Mbunge wa Viti Maalum 2007 ambapo alihugumu 2010.
Pia marehemu Getrude amekuwa kada wa muhimu CCM kwa miaka mingi hadi anakutwa na umauti.

No comments:

Post a Comment

Pages