HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 17, 2020

UJENZI WA DARAJA JIPYA LA MTO WAMI KUWAKOMBOA WANANCHI KIUCHUMI, KUPUNGUZA AJALI

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara wa (wa pili kulia), ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akioneshwa na mmoja wa wahandisi moja ya ramani ambayo inatumika katika mradi  mkubwa wa ujenzi wa daraja la mto wami ambalo linajengwa kwa fedha za serikali baada ya kufanya ziara yake ya kikazi kwa ajili ya kujionea shughuli mbali mbali zinazofanyika katika eneo hilo.


Baadhi ya viongozi wa Serikali wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarst Ndkilo wa kati kati mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa daraja jipya linalojengwa katika eneo la mto Wami. Kushoto kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainabu Kawawa na kulia kwake ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Bagamoyo.

 

 

VICTOR MASANGU, BAGAMOYO  

 

IMEELEZWA kuwa wimbi la ajali za barabarani ambazo zilikuwa zikitokea mara kwa mara katika eneo la daraja la Mto Wami lililopo Wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani na kupelekea baadhi ya watu kupoteza maisha  yao na wengine kupata vilema vya kudumu  huenda changamoto hiyo ikabaki kuwa ni historia pindi utakapokamilika mradi  wa ujenzi wa daraja  jipya Septema 16, 2021.

 

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara ambaye pia ni  Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kutembelea miundombinu ya barabara pamoja ambapo amesema kwamba kukamilika kwa ujenzi wa mradi mkubwa wa daraja la mto wami utakuwa ni mkombozi mkubwa wa kumaliza changamoto  zilizokuwa zikiwakabili wasafiri wanaotumia njia hiyo.

 

Ndikilo alifafanua kwamba hapo awali katika eneo hilo kulikuwa na matukio mbali mbali ya magari kupata ajali lakini ana imani endapo mradi huo pindi utakapokuja kukamilika hapo septemba mwakani utaweza kuwasaidia wasafiri wengine sana wa ndani na nje ya nchi kwani serikali imeamua kuweka mikakati ya kumaliza kabisa hali hiyo.

 

“Mimi kama Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara na pia ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani tumeamua kufanya ziara maalumu yenye lengo la kuweza kutembelea miradi mbali mbali ya miundombinu ya barabara ambayo inajengwa pamoja na kujionea madaraja katika maeneo tofauti ikiwemo daraja la mto wami ambalo ndilo serikali imeweza kutoa fedha zake kwa asilimia mia moja kwa nia njema kabisa ya kuwasaidia wananchi,”alisema Ndikilo.

 

Pia mkuu huyo wa mkoa alisema kwamba kukamilika kwa ujenzi wa daraja hilo kutaweza kutoa fursa mbali mbali za wafanyabiashara ambao walikuwa wanasafirisha bidhaa zao na kwamba kutaweza kuleta mabadiliko chanya  ya kimaendeleo kwani fursa nyingine zitaweza kupatikana kutokana na barabarara hiyo ambayo inaunganisha baadhi ya mikoa pamoja na nchi nyingine za jirani.

 

Katika hatua nyingine Ndikilo aliwaagiza wakandarasi wa mradi huo kufanya jitihada za makusudi za usiku na mchana ili kuhakikisha kwamba wanamaliza kukamilisha ujenzi huo kwa muda amabao umepangwa lengo ikiwa ni kumaliza kabisa changamoto ya kupita katika eneo hilo ambalo limekuwa na historia ya kutokea kwa ajali za mara kwa mara.

 

 Kwa upande wake   Mhandisi mshauri kutoka  kampuni ya Ilshin ya Korea inayojenga mradi wa huo Gabriel Sangusangu amebainisha kuwa daraja hilo ambalo lina urefu wa mita 510 na upana wa mita 11.87 limegharimu kiasi cha shilingi bilioni 67.8 ambazo zote zimetolewa na serikali ya Tanzania.

  

“Ujenzi huu wa daraja la mto wami kwa sasa unaendelea vizuri kama mnavyoona na kitu kikubwa ambacho tunakifanya kwa sasaa ni kuhakikisha tunafanya kazi kwa bidii usiku na mchana ili tuendane na tarehe ambayo tumepangiwa ya septemba mwakani na uzuri fedha zote zimetolewa na serikali yetu ya awamu ya  tano ili kuboresha miundombinu ya barabarara.”alisema Mhandisi huyo.

 

Naye Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Zainabu Kawawa alisema kwamba uwepo wa daraja hilo la mto wami utaweza kuwaletea wananchi maendeleo makubwa kwani hapo awali walikuwa wanasumbuka sana kutokana na njia hiyo kuwa finyu hivyo walikuwa wanapita kwa shida sana na baadhi ya magari kupata ajali.

 

Nao baadhi ya wananchi Wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani walitoa pongeza kwa serikali ya awamu ya tano kwa kuweka mipango madhubuti ya kuboresha miundombinu mbali mbali ya barabara pamoja na madaraja huku wakiiomba zaidi kuwaboresha barabara zao za vijijini ili ziweze kupitika kwa urahisi nyakati za mvua.

No comments:

Post a Comment

Pages