Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa ameliagiza Shirika la Reli Tanzania (TRC) kuhakikisha linasimamia Ujenzi wa Jengo la Stesheni ya Reli ya Kisasa ya Dar es salaam-SGR la Tanzanite kukamilika kwa wakati kabla ya mwezi wanne mwaka huu.
Ameyasema hayo leo jijini Dar es salaam wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya jengo la stesheni hiyo akiwa ameambata na Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Mhandisi Masanja Kadogosa pamoja na wafanyakazi wa TRC.
Profesa Mbarawa ametoa maelekezo kuwa jengo hilo limalizike kwa haraka lakini pia litakapoanza kutumika liwekewe usimamizi mzuri ili liendelee kuwa katika ubora wake.
Amebainisha kuwa wakati umefika jengo hilo liweze kumalizika na sio kuahidi kila wakati hivyo mpaka mwezi wa nne mwaka huu ni vyema likakamilika.
Amelisistiza shirika hilo kuweka utaratibu wa kulifanyia ukarabati jengo hilo mara kwa mara ili liweze kudumu kwa muda mrefu na hivyo kuonekana kuwa la mfano kwa wageni mbalimbali pamoja na wananchi pindi wanapolitembelea.
"Hili jengo ni zuri sana kwani limejengwa kwa miundombinu mizuri hivyo ni lazima tuwe na utamaduni kulifanyia ukarabati wa kuja kulisimamia vinginevyo miaka miwili au mitatu litakuwa halitamaniki lazima tubadilike",amesema Profesa Mbarawa.
Ameliagiza na kulitaka TRC kubadilika katika utoaji wa huduma wa SGR tofauti na treni ya zamani ili watu waone utofauti wa kuwa treni hiyo ni ya kisasa kwani kufanya hivyo watapata heshima kubwa kwa watanzania.
Amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zinazoendelea kusaidia ujenzi wa miundombinu ya treni ya SGR
No comments:
Post a Comment