HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 30, 2022

SMZ kuwa na Umeme wa Uhakika Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inaendelea kujikita katika kutekeleza mipango ya uhakika ya upatikanaji wa nishati mbadala kwa kwaajili ya maendeleo endelevu Zanzibar kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa nje na ndani ya nchi.

Akiwasilisha mada ya nishati mbadala katika jukwaa la uwekezaji upatikanaji wa nishati mbadala Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa  Wizara ya Maji na Nishati, Madini, Dkt Mngereza Mzee Miraji,  amesema mipango inayoendelea Tanzania katika kusambaza umeme vijijini inalenga kuimarisha  maisha na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi kupitia upatikanaji wa nishati ya umeme wa uhakika.

Dkt Mngereza alisema, Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2050 inaeleza mahitaji ya mfumo wa nishati ya uhakika kupitia vyanzo mbalimbali vya nishati, hasa nishati mbadala.

Aidha alisema Benki ya Dunia inaisaidia Zanzibar kutekeleza mradi wa Kuifanyia Mabadiliko Sekta ya Nishati - ZESTA ili kutatua changamoto za upatikanaji umeme kisiwani humo.

Alifahamisha kwamba kukamilika kwa mradi wa ZESTA kutapanua upatikanaji wa huduma za umeme wa uhakika na wenye ufanisi ili kuongeza uzalishaji wa nishati mbadala ikiwemo kuzalisha 18MW za umeme wa jua.

Alisema, mradi huo ni mradi wa miaka mitano unaotekelezwa kwa gharama ya dola Milioni 142 kutoka Benki ya Dunia na utakapokamilika utanufaisha watu 300,800 katika kisiwa cha Zanzibar.

Aidha amefafanua kuwa, ukuaji wa sekta ya nishati unatarajiwa kuchangia na kukuza ukuaji wa uchumi, huduma za jamii pamoja na kuvutia wawekezaji.

“Juhudi kubwa zimechukuliwa na Serikali kuhakikisha Zanzibar inakuwa na vyanzo vyake vya ndani vya kuzalisha umeme ambapo matumizi ya nishati ya jua yameongezeka kwa asilimia 6.1 mwaka 2019-2020 ambapo lengo ni kufikia asilimia 20 ifikapo mwaka 2030,” alisema Dkt Mgereza.

Dkt Mgereza aliongeza kuwa Visiwa vya Kokota na Njau, kisiwani Pemba vimeunganishwa na umeme wa jua wa KW 130 ambayo unanufaisha zaidi ya Kaya 140, mradi huo umesaidia kuondoa changamoto ya nishati ya umeme katika visiwa hivyo, umetekelezwa kwa ushirikiano ya SMZ na Serikali ya Norway kwa gharama ya dola za Marekani 458,000.

Naye Meneja Mwakilishi kutoka katika mradi wa nishati katika nchi za Umoja wa Ulaya, Massimiliano Pedretti, ameihakikishia serikali ya Tanzania kuwa nchi hizo zitaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuleta maendeleo endelevu katika sekta ya uchumi na jamii.

Jukwaa hilo la siku tatu lililoshirikisha wadau kutoka nchi mbali mbali ikiwa ni pamoja na Congo DRC, Uganda na Msumbuji, lilifunguliwa na Waziri wa Nishati, January Makamba, ambapo wadau walijadili mafanikio na changamoto zinazoikabili sekta ya nishati katika nchi zao.


No comments:

Post a Comment

Pages