HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 12, 2023

RAIS SAMIA, MBOWE, ZITTO WAMLILIA MEMBE

Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi mbalimbali wametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, aliyefariki katika Hospitali ya Kairuki mkoani Dar es Salaam.



Hizi ni baadhi ya jumbe mbalimbali walizoandika viongozi hao kupitia kurasa zao za mitandao ya kijamii (Twitter).

"Nimepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Ndugu Bernard Membe. Kwa zaidi ya miaka 40, Ndugu Membe alikuwa mtumishi mahiri wa umma, mwanadiplomasia, Mbunge na Waziri aliyeitumikia nchi yetu kwa weledi. Pole kwa familia, ndugu, jamaa & marafiki. Mungu amweke mahali pema. Amina". Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.



"Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje Mheshimiwa Bernard Membe. Mheshimiwa Membe aliitumikia nchi yetu katika ngazi mbalimbali na alikua hazina muhimu kwa Taifa. Raha ya milele umpe ee bwana, na mwanga wa milele umuangazie". Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.



"Hakuna maneno yanayoweza kueleza mstuko mkubwa nilioupata kufuatia Taarifa ya msiba huu, zaidi ya kumshukuru Mungu muumba kwa Maisha ya Mzee wetu Bernard Kamilius Membe ambaye amefariki Dunia Leo asubuhi. Mwanasiasa mahiri, mwanadiplomasia maarufu na mwakilishi wa Wananchi". Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe.




"Ni HABARI ngumu sana kuipokea na kuikubali. Lakini UKWELI ni kwamba SOTE tuko NJIANI kukufuata huko ULIKO. Duniani TUNAPITA tu. Upumzike kwa AMANI, Baba, Kaka, RAFIKI na NDUGU yetu BERNARD KAMILIUS MEMBE. Pole sana KWA FAMILIA, MAMA YETU na WATOTO." Mbunge wa Viti Maalum Chadema, Halima Mdee.

"Innaillah Wainalailah Rajeun, nimepoteza mtu muhimu sana.Mungu akulaze mahali pema Mzee wangu, Bernard Camilius Membe. Kwangu wewe ulikuwa ni mzazi, mlezi na mshauri wangu katika siasa ukiwa ndani ya chama chetu hata nje ya chama chetu uliendelea kunielea,Siamini leo umetuacha". Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana ACT-Wazalendo, Abdul Nondo.


No comments:

Post a Comment

Pages