HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 27, 2023

TANI 700 ZA SALFA ZIMEPOKELEWA PWANI

Baadhi ya wakulima wa zao la ufuta wakiwa kwenye  mnada.


 

Na Khadija Kalili 

 
SERIKALI Imefikisha Tani  700 za viuatilifu aina ya Salfa kwenye Chama Kikuu Cha Wakulima  Mkoa wa Pwani CORECU kwa ajili ya zoezi la usambazaji kwa wakulima wa zao la korosho linaloendelea Mkoani humo.

Akizungumza na baadhi ya wakulima wa Mkoa huo kwenye mnada wa saba wa ufuta uliofanyika  katika ghala kuu la Wilaya ya Kibiti Meneja wa CORECU Mantawela Hamisi amesema
maandalizi ya msimu wa zao la korosho kwa mwaka 2023 yameanza ambapo wakulima wameshaanza kupokea na kuanza kupulizia mikorosho yao  viuatilifu vyao aina ya Salfa ya unga na ya maji.

Amesema   matarajio waliyonayo  ni  kuwa  Mkoa mzima wa Pwani kupitia Bodi ya Korosho Tanzania  CBT na Chama hicho kikuu  ni kupokea tani 1,000 ambazo zinaendelea kugaiwa kwa wakulima kiwilaya na Kata kulingana na Wakulima walivyojiorodhesha kwenye mfumo kupitia Maafisa Kilimo wao.

Amesema Tani 300 zingine bado hazijafika hivyo amewaomba wakulima kuwa wavumilivu  na kusubiri kiasi hicho cha Salfa ambayo bado haijafika.

"Pindizitakapofika zinapokelewa kwenye mfumo ndipo watu wa Bodi ya Korosho Tanzania wanazichakata na kutoa maelekezo ya jinsi ya kugawana Salfa hiyo kulingana na mfumo unavyopanga"

"Yaani kadri Salfa zinavyoingia, ndivyo zinavyoingizwa kwenye mfumo na jinsi mfumo unavyogawa ndipo na sisi CORECU ndivyo tunavyowaletea Wakulima pembejeo zenu" amesema Hamisi.

Amesema usambazaji wa pembejeo hizo unaendelea katika Mkoa mzima wa Pwani  na  ameonesha magariaina ya  malori yakipakia pembejeo hizo kuzipeleka katika Wilaya za Kisarawe, Mkuranga, Bagamoyo, Kibaha, Kibiti na Rufiji.

 Meneja huyo ameonesha kushangazwa na mutikio mdogo wa wakulima kujisajili katika mfumo wa pembejeo kutoka katika Wilaya za Kibiti na Rufiji ambao ndiyo wamekuwa wakulima wakubwa wa mazao ya ufuta na Korosho na kujisababishia kupata mgao mdogo wa pembejeo hizo tofauti na Wilaya ya Mkuranga ambayo Wakulima wake wamejisajili kwa wingi hivyo wengi watapata pembejeo kuliko Wilaya zote za  Mkoa wa Pwani.

"Mkuranga wameitikia zaidi kuliko Kibiti na Rufiji ambapo Wilaya ya Kibiti kuna Wakulima wengi zaidi,hivyo msijemkashangaa usambazaji wa pembejeo Wilaya ya Mkuranga ikawa imepokea pembejeo nyingi kuliko Wilaya ya Kibiti kwasababu wenzetu wameitikia kujisajili lakini huku sijui mlikuwa mnakwama  wapi ?"

"Sasa madhara yake utasikia watu wana namba lakini hamjapata pembejeo ni kwakuwa hamkujisajili kwa wakati na muda umeshakwenda hivyo ninyi mliokuwa mkijivuta vuta ntakuja kupewa baadaye sana na endapo  zikiisha tusijetukalaumiana"

Aidha Hamisi amesema pembejeo hizo serikali inazigawa kwa ruzuku ambapo mkulima hachangii kiasi chochote cha fedha lakini hazitatosheleza kila mkulima.

"Pembejeo hizo hazitatosheleza kila mkulima kwasababu pembejeo huletwa kwa namna mkulima alivyojisajili kwenye mfumo wa pembejeo".

"Mfuko mmoja wa Salfa utapulizia kwenye miti mia ya mikorosho sasa kama wewe una miche mingi kuliko pembejeo ulizopewa maana yake ni kwamba pale serikali ilipoishia kukusambazia unaruhusiwa kwenda kujitafutia sehemu nyingine kwa sababu serikali haiwezi kumuhudumia mkulima kwa mahitaji yake yote"

Pia amewataka Maofisa Kilimo waliohusika katika kusajili wakulima kwenye mfumo huo kwa kushirikiana na uongozi wa AMCOS za Kata husika wahakikishe wakulima wao wanapata pembejeo zao kama walivyojiandikisha.

Amesema bei ya ufuta iliyopitishwa katika mnada huo kuwa ni shilingi 3,805.34 kwa kilo moja.

No comments:

Post a Comment

Pages