HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 22, 2024

The Foundation for Civil Society na TradeMark Africa wasaini Makubaliano Mradi wa kutetea Haki za Walaji, Mazingira wezeshi na Ujumuishi Kibiashara

Na Hussein Ndubikile, Dar es Salaam


Shirika lisilo la Kiserikali laThe Foundation for Civil Society (FCS) na TradeMark Africa (TMA)  yamesaini makubaliano ya utekelezaji wa Mradi wa kuboresha mazingira wezeshi na jumuishi ya kibiashara yenye lengo la kuhakikisha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu wanajumuishwa kikamilifu katika uendeshaji wa biashara. 


Makubaliano hayo pia yana lengo la kuyawezesha makundi hayo kukabiliana na changamoto kubwa za kimfumo na tabianchi kama sehemu ya kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi Tanzania.

FCS imepokea ruzuku ya Sh Bilioni 2.3 kutoka TradeMark Africa kutekeleza mradi huu ambao umefadhiliwa na Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo (FCDO), Ireland na Norway ambazo zimetoa dola za Kimarekani 900,000. Mradi pia unalenga kuunganisha nguvu za sekta binafsi na mashirika ya kiraia ili kukuza ukuaji wa uchumi wa kijani.

Tafiti zinaonyesha kwamba wanawake wanaweza kutoa mchango mkubwa wa kiuchumi kama wakishirikishwa kikamilifu katika mifumo ya biashara. Hata hivyo, wanawake wengi nchini Tanzania bado wanakumbana na vikwazo vingi vinavyowazuia kushiriki kikamilifu katika sekta ya biashara. 

Mradi huu unalenga kukabiliana na vizuizi hivi na kuweka mazingira wezeshi ya biashara ambayo yanajumuisha watu wote na kukuza ustawi wa wote.Mradi huu ni wa kipekee na utajumuisha sekta binafsi pamoja na asasi za kiraia ili kuimarisha biashara ambayo ni ya umoja na endelevu ya mazingira. Katika kipindi cha miezi 18 ijayo, FCS itatekeleza mkakati katika sekta nyingi za biashara, ikilenga kupunguza athari za matumizi ya mazingira na kukuza ushirikishwaji katika manufaa ya kiuchumi.

Akizungumza  na wanahabari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkazi wa TradeMark Africa, Elibariki Shammy, amesema, “Mradi huu ni muhimu kwa malengo yetu ya kimkakati ya kuchochea ukuaji wa biashara ambao ni endelevu na shirikishi. Tunaamini kwamba kupitia  ushirikiano huu wa kimkakati baina yetu na FCS, tunaweza kuleta matokeo chanya na makubwa katika kuboresha mazingira ya biashara jumuisha nchini. Kuwawezesha wanawake ni jambo la maendeleo. Kuwajumuisha wanawake katika biashara kunakuza uchumi na kuinua jamii nzima. Kupitia mradi huu na ushirikiano baina yetu na FCS, tunalenga kuendeleza mfumo bora wa biashara ambao unajumuisha na unaoweza kukabiliana na changamoto za biashara ya kimataifa.”

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa FCS, Justice Rutenge, ameelezea umuhimu wa mradi huo."Ulinzi wa mlaji ni muhimu sana katika soko la biashara la kitaifa na kimataifa. Ushirikiano wetu na TradeMark Africa ni hatua kubwa ya kulinda haki za mlaji nchini na kuwezesha mazingira wezeshi ya kibiashara yaliyo bora na yanayokabiliana na changamoto za tabianchi nchini. Tutahakikisha kwamba faida za biashara ni shirikishi na zinanufaisha wananchi wote katika jamii yetu,” amesema.

Amebainisha kuwa FCS ina jukumu la kipekee kama AZAKI na itaweza kutumia vyema ubobezi wake katika sekta kushirikiana na sekta binafsi kushughulikia masuala muhimu ya uharibifu wa mazingira na ukosefu wa usawa katika kijamii. 

Amesisitiza kuwa mradi huo unalenga kuweka mazingira ya biashara ambayo ni jumuishi na endelevu kwa kuongeza fursa za kibiashara kwa makundi ya pembezoni, kushirikiana na asasi za kiraia kushughulikia mahitaji yao, kukuza mazingira ya biashara rafiki na kuimarisha ulinzi wa
walaji.

Ameongeza kuwa TMA itasadia jamii za pembezoni kupitia kilimo-mahiri na programu za masoko na kuchangia ukuaji endelevu wa biashara zao. Aidha, kwa kutetea ukuaji wa biashara endelevu, mradi huu unalenga kuboresha ustahimilivu wa biashara dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na hivyo kuchangia katika uendelevu wa muda mrefu wa uchumi wa Tanzania na uendelevu wa mazingira.

Amefafanua kuwa mradi pia unajumuisha matumizi ya teknolojia za kibunifu za kidijitali kama vile majukwaa ya kujifunza kielektroniki mbinu za kilimo mahiri, kuimarisha utayari wa soko naushindani wa kimataifa wa bidhaa za Tanzania.

Pia amesema makubaliano hayo ni kielelezo tosha cha jinsi ushirikiano wa sekta za umma na binafsi unavyoweza kushughulikia kwa ufanisi changamoto za kimfumo katika masoko ibuka na kuunda njia za mazoea ya biashara jumuishi na endelevu.

No comments:

Post a Comment

Pages