Shauri la Mapitio Namba 32537 la 2025 la kupinga uundwaji wa Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea nchini wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba 2025 lilifunguliwa Mahakama Kuu masjala ndogo ya Dar es salaam na Rosemary Mwakitwange na wenzake watatu dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) pamoja na Wajumbe wa Tume hiyo ya Uchunguzi.
Katika shauri hilo, waleta maombi waliiomba Mahakama Kuu, kupitia utaratibu wa mapitio (Judicial Review), itoe amri ya kufuta uamuzi wa Mheshimiwa Rais wa kuunda na kuteua wajumbe wa Tume hiyo tarehe 18 Novemba, 2025 wakidai kuwa Rais alivuka mipaka ya mamlaka yake ya kisheria wakati wa kuunda Tume hiyo.
Shauri hilo liliendeshwa na kusimamiwa na jopo la Mawakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa niaba ya Serikali.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, tarehe 13 Machi 2026, Mahakama Kuu imetupilia mbali shauri hilo, ikieleza kuwa Mheshimiwa Rais alitumia mamlaka aliyonayo kisheria chini ya Kifungu cha 3 cha Sheria ya Tume za Uchunguzi, Sura ya 32, na kwamba hakuvunja mamlaka yake ya kisheria katika kuunda Tume hiyo.
Mahakama imeeleza kuwa kwa mujibu wa Kifungu cha 3 cha Sheria ya Tume za Uchunguzi,sura 32 Rais ana mamlaka ya kuunda Tume na kuteua wajumbe wake.
Mahakama pia imebainisha kuwa hakuna ushahidi uliowasilishwa mahakamani unaoonesha kuwa Rais alienda kinyume na matakwa ya sheria hiyo wakati wa kuunda Tume. Aidha, Mahakama haikuona uwepo wa upendeleo (bias) katika uteuzi wa wajumbe wa Tume, kwa kuwa sheria inampa Rais mamlaka ya kufanya uteuzi huo.
Kutokana na sababu hizo, Mahakama imehitimisha kuwa maombi ya walalamikaji hayakuwa na msingi wa kisheria, hivyo yakatupiliwa mbali.





No comments:
Post a Comment