HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 19, 2013

TABOA KUKUTANA NA MKURUGENZI WA JIJI LA DAR ES SALAAM LEO


Na Mwandishi Wetu

CHAMA cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA), kinatarajia kukutana na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam pamoja na Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA), leo ili kujadili tatizo la wapiga debe katika Kituo kikuu cha Mabasi cha ubungo.

Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa waiki jijini Dar es Salaam, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Taboa Rajab Kassim, alisema tatizo la wapigadebe kituoni hapo ni asilimia themanini, bado kuna haja ya kukutana na wadau hao ili kulitafutia ufumbuzi wa kudumu si wazima moto.

Alisema wanatarajia majadiliano hayo yatasaidia kuleta suluhu katika kampeni za kuwaondoa wapi gadebe kituoni hapo, kufuatia operesheni ya kwanza iliyofanywa na askari wa ulinzi shirikishi wa chama hicho kwa wakishirikiana na  askari wa Jiji, kuleta mafanikio hayo.

“Operesheni hiyo ya wiki mbili hadi sasa, kwa kiasi kikubwa imefanikiwa kuwaondoa wapigadebe hao ambao kwa kipindi kirefu walikuwa kero kwa abiria, mkutano wetu wa leo na Mkurugenzi pamoja na Sumatra utatusaidia kufikia malengo tulioyakusudia” alisisitiza Kassim.

Alisema kutokana na kero ya wapigadebe hao iliyokuwa kama ‘mwiba mchungu’ kwa uongozi wa Jiji la Dar es salaam, Taboa iliamua kuweka mkakati maalumu ulioshirikisha Polisi, Halmashauri ya Jiji na askari wa ulinzi shirikishi waliopo chini ya Chama hicho.

“Tumeliona jambo hili ndiyo jukumu letu kubwa katika mipango yetu ya kuboresha huduma za usafiri, ikumbukwe ni kipindi kirefu kimepita tangua tatizo la wapigadebe hawa lianze kulalamikiwa, mikakati ni kuwaondoa kabisa wapigadebe hao katika eneo la kituo” alisema Kassim.

Aidha Kassim alisema kuondolewa kwa wapigadebe hao kwa kiasi kikubwa kumeondoa adha kwa abiria waliokuwa wakifika hapo kwa ajili ya kupatiwa huduma ya tiketi ambao mara nyingi walijikutwa wakiibiwa mali zao kutokana na kuvutwavutwa pasipo na ridhaa yao.

“Tunawashauri wamiliki wa mabasi kuachana na wapigadebe hawa na kujiandaa na utaratibu mpya wa ukataji wa tiketi kwa njia ya mtandao maarufu kama ‘E-Bus Ticketing’ unaotarajiwa kuanza hivi karibuni mara baada ya marekebisho katika mtandao yatakapokuwa yamekamilika” aliongeza Kassim.

No comments:

Post a Comment

Pages