HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 16, 2013

VIJANA WA TANZANIA WASHAURIWA KUWA WABUNIFU

Na Elizabeth John


VIJANA wa Kitanzania wameshauriwa kutobweteka badala yake wajishughulishe na kazi mbalimbali sio kutegemea ajira za serikalini pekeee.


Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Mchoraji wa michoro ya Tingatinga, Abbas Mbuka na kwamba yeye anajivunia kuwa mchoraji wa michoro hiyo kutokana na faida anazozipata.

“Mimi nawashauri watanzania wenzangu wafanye kazi mbalimbali na sio kukaa tu mitaani kama wanavyofanya vijana wengi, mimi napata kipato cha kunitosheleza kupitia kazi hii kinachotakiwa ni ubunifu tu,” alisema.

Alisema kupitia kazi hiyo aliweza kuhudhulia mkutano wa tano wa kuzungumzia Maendeleo ya nchi za Afrika ujulikanao kama Tokyo International Conference on African Development (TICAD - V) mjini Yokohama, Japan ambapo aliweza kuonesha jinsi ya kuchora michoro hiyo pamoja na kuziuza kwa raia wa huko.

Alisema mkutano huo uliwashirikisha viongozi wa Afrika akiwemo Rais Jakaya Kikwete, viongozi wa Japan na mashirika ya maendeleo ya Afrika ikiwamo Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU) na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP).

Alisema awali picha za michoro hiyo ya Tingatinga ilianza kuuzwa Fukohama, Goya ambapo waliuza picha 160, Wosaka waliuza picha zaidi ya 100 na Yokohama waliuza picha zaidi ya 220.

Alisema lengo la picha hizo kupelekwa nchini Japan ni kuonyesha vitu mbalimbali vinavyopatikana Afrika kupitia michoro ya sanaa hiyo ya Tingatinga.

Alisema katika mkutano huo, kila nchi ilikuwa inaonyesha bidhaa zao, hivyo na wao walipata fulsa ya kuonyesha za kwao, na kufanikiwa kuuzika zaidi na walivyotarajia.

Mbuka alisema bado nchini humo kuna watu ambao wanaona wanyama kwenye luninga, hivyo kuona kwao katika michoro kunawafanya wajifunze mengi zaidi kutoka Afrika.

“Wasanii wa Tingatinga tunaweza kufika mbali sana, kwani michoro yetu inakubalika kila nchi na hii itawafanya pia watu waamini kuwa michiro ya Tingatinga imetokea Dar es Salaam Tanzania na si nchi nyingine kama watu wanavyosema,” alisema Mbuka.

No comments:

Post a Comment

Pages