HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 25, 2015

Familia yaridhia ndugu yao kuuawa

Na Mwandishi Wetu, Mvomero

BAADA ya wananchi, viongozi wa siasa, serikali, dini na polisi mkoani Morogoro kushusha pumzi ya kuona matukio ya wizi sugu wa jambazi la kutisha, Frank Mwambaswa, maarufu kama Geuka, hata familia yake haikumuingiza nyumbani ili aagwe wala kumuwekea matanga.

Mwambalaswa aliuawa kwa kuchomwa mishale miwili majira ya usiku hivi karibuni kijijini kwake (Kunke), Kata ya Mtibwa, Wilaya ya Mvomero, pale alipovunja na kuingia kuiba dukani kwa Stephen Sanga, ambaye amekuwa akimwibia kila mara na kuahidi kuwaua yeye na mkewe.

Sababu za kuwaibia na kutaka kuwaua zilibainika kwenye msiba huo kuwa ni kutokana na wao kumkodisha mashine ya kukatia mbao (chain saw), ambapo kila walipomuulizia kuhusu malipo hata kupitia kwa ndugu zake, alitoa vitisho hivyo kwa ndugu zake, ambao waliogopa kumwambia mdai.

Siku ya tukio, Mwambalaswa ambaye mwaka 1993 alifungwa miaka 15 jela kwa makosa kama hayo na uuaji, alivunja nyumba ya Sanga na kuingia ndani, ambapo alibeba vitu vya kwanza ikiwemo jenereta na kuviweka nje, na aliporudia vingine ili hatimaye awaue Sanga na mkewe, walinzi walimpiga mishale miwili.

Mwambalaswa alijitahidi kukimbia na mishale hiyo, lakini sumu yake ilimfanya akate roho kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Kunke, ambapo alifuatwa na kuburuzwa hadi kwenye vitu alivyoiba.

Jeshi la Polisi kwa upande wake, baada ya kupewa taarifa hizo na kuthibitisha wizi uliofanywa, lilifanya taratibu zinazostahili na kuamuru familia imzike marehemu, ambapo familia haikutaka hata aingizwe ndani, bali waliamuru azikwe na kutangaza kuwa hakutakuwa na matanga.

Aidha, wananchi, viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini na makundi mbalimbali ya kutetea haki za binadamu, yalikuwa na kigugumizi kutetea suala hilo, badala yake walilaani  tabia ya marehemu, ambaye kimsingi aliogopwa.

Watu mbalimbali walioibiwa na kufanyiwa unyama na jambazi huyo walikuwa wakishangilia, huku wakiionya jamii kuwa malipo ya matendo mabaya yapo hapa hapa duniani.

No comments:

Post a Comment

Pages