HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 25, 2015

WANAHARAKATI WA TANZANIA WANATOA WITO KWA JAMII KUCHUKUA HATUA ILI KUMLINDA MTOTO APATE ELIMU BORA NA SALAMA

 Dr. Judith Odunga Mkurugenzi wa Shirika la WiLDAF akisoma taarifa kwa vyombo vya habari kuhusiana na kuanza kwa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.

FUNGUKA! CHUKUA HATUA MLINDE MTOTO APATE ELIMU

Katika kuadhimisha Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia kuanzia tarehe 25 Novemba mpaka 10 Desemba, WiLDAF, Mashirika ya Haki za Binadamu, Wadau wa Maendeleo na Asasi za Kiraia watatoa elimu na kuhamasisha umma kuchukua hatua kumlinda mtoto ili apate elimu bora na salama. Ulinzi wa mtoto ni pamoja na kuzuia vitendo vyote  vya ukatili wa kijinsia.

Maadhismisho ya SIku 16 za kupinga Ukatili wa kijinsia mwaka huu yanalenga zaidi kuzungumzia suala zima la usalama  mashuleni, lengo kuu ikiwa kuhamasisha umma kuhusu ukubwa wa tatizo la ukatili wa kijinsia kwa vijana na watoto wetu mashuleni, kwani vitendo vingi vya ukatili wa kijinsa vimekuwa vikiripotiwa.

Utafiti uliyofanywa na Chuo cha Tiba Cha Muhimbili (MUHAS) kwa kushirikiana na Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika, (WiLDAF) umetambua hatari zinazochangia ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na wazazi kutowajali watoto na kutoa adhabu kali kwao na hivyo kuwafanya watoto kuwa na hofu. Wakati mwingine watoto kufanyiwa ukatili bila wao kufahamu. Aidha, adhabu ya viboko inahusishwa kama moja ya aina za ukatili dhidi ya watoto. Hii inaathiri maendeleo ya elimu ya watoto katika taifa letu.

Kukosekana kwa usawa kati ya watoto wa kiume na wa kike hunapelekea kuwajengea hofu watoto wa kike,  na wakati huo kuwajengea watoto wa kiume ujasiri wa kuona kuwa ni sahihi kwao kufanya  vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Aidha, tafiti kuhusu Ukatili Dhidi ya Watoto (VAC) uliofanywa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia watoto (UNICEF) wa mwaka 2011 ulionesha kwamba watoto 3 wa kike kati ya 10 na mtoto 1 kati ya watoto 7 wa kiume wenye umri kati ya miaka 13-24 wamewahi kufanyiwa ukatili wa kingono. Aidha, asilimia 6 ya watoto wa kike wamelazimishwa kufanya tendo la ngono kabla ya miaka 18. Pia utafiti huo unaonesha kuwa watoto wa kike wanafanyiwa vitendo vya kingono  na wanaume waliowazidi umri wakati watoto wa kiume wanafanyiwa ukatili na watoto wenye umri sawa.

Tafiti pia imeonesha kuwa vitendo hivyo vinafanywa na watu wanaowafahamu wakiwemo majirani, wapenzi wao, watu wenye mamlaka (walimu). Ni  asilimia 32.2 tu ya watoto wa kike na asilimia 16.6 ya watoto wa kiume wamefanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na watu wasiofahamika na watoto. Vitendo hivi hufanyika maeneo ambayo uangalizi wa watu wazima unahitajika kuwepo kwa mfano mashuleni, njiani, majumbani na wakati mwingine katika vyombo vya usafiri.

Ni dhahiri kwamba kwa mazingira, mila na utamaduni ikijumuisha familia za Kitanzania, vimekuwa vikichangia vitendo vya ukatili wa kijinsia. Vitendo vya ukatili na udhalilishaji vina madhara makubwa ya kiafya kwa watoto kwani hukatisha uwezo wao wa kielimu, mahudhurio ya shule na hivyo kupelekea matokeo mabaya ya  katika ufaulu wao wakati wa mitihani.

Aidha, mazingira yasiyo salama kwa watoto wa shule yana madhara makubwa. Watoto wanapokuwa mashuleni na kufanyiwa ukatili wa kingono wapo katika hatari kubwa zaidi ya kupata maambukizi ya UKIMWI kwa mathlani mara tatu zaidi ya wale ambao hawajawahi kufanyiwa ukatili.

Tunaamini kwamba kuondolewa kwa vikwazo vinavyo chochea ukatili wa kijinsia kwa watoto wa shule kutachangia katika kuleta usawa wa kijinsia kwa watoto wa kiume na wa kike. Pia mazingira mazuri ya shule yatasaidia mahudhurio mazuri ya watoto mashuleni na  kuleta matokeo mazuri katika ufaulu.

Jamii inahaswa kuweka mazingira mazuri ya shule ikiwa ni pamoja na kuwepo miundombinu kama mabweni, vyoo, madawati, uzio kuzunguka mashule na vyombo rafiki vya usafiri. Haya yote yatawezekana tu ikiwa kutakuwa na dhamira ya dhati kwa watunga sera, wazazi, walimu, wanafunzi na jamii kwa ujumla katika kuzuia ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto. Kuna haja ya makusudi kabisakutofumbia macho  masuala ya ukatili kwa ujumla wake ili kujenga jamii imara.

Siku 16 za Kupinga ukatili wa kijinsia  ni tukio la kimataifa la kila mwaka ili kuwa na nguvu ya pamoja  katika kuzuia kuenea kwa janga hili . Ndani ya siku hizi, kuna siku zingine muhimu za kimataifa , mathlani, Novemba 25 ni Siku ya Kimataifa ya Kupinga Ukatili Dhidi ya Wanawake, Novemba 29 ni Siku ya Kimataifa ya Watetezi wa Haki za Binadamu, Desemba 1 ni Siku ya UKIMWI Duniani, Desemba 3 ni Siku ya Kimataifa ya watu wenye Ulemavu, Desemba 6 ni Siku ya Kimataifa ya Kumbukumbu ya Mauaji ya kikatili ya Montreal 1989, ambapo wanawake 14 waliuawa na mtu aliyekuwa anawachukia wanawake. Tarehe hizi zilichaguliwa mahususi ili kuhusianisha kwamba ukatili wa kijinsia unaongeza maambukizi ya UKIMWI na ni Ukiukwaji wa Haki za Binadamu.

Katika kipindi hiki cha Kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia , mamia ya asasi za kiraia na wadau mbalimbali Tanzania wataifikia jamii kwa kauli mbiu inayosema;
FUNGUKA! CHUKUA HATUA MLINDE MTOTO APATE ELIMU.

No comments:

Post a Comment

Pages