*Atoa miezi miwili Wizara ya Habari ikamilishe mchakato wa vazi la Taifa
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa muda wa miezi miwili na nusu kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezoiwe imekamilisha mchakato wa Tanzania kuwa na vazi la Taifa.
Amesema
 Watanzania bado hawajaunganishwa kwa kuwa na vazi la Taifa, ambalo 
mchakato wake  umeendeshwa kwa miaka mingi na wizara hiyo bila ya 
kujulikana wamefikia wapi.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Oktoba 13, 2018) wakati akifunga tamasha za Urithi Festival, lililofanyika kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini  Arusha.
“Ifikapo
 Desemba 30,2018 tuwe tumeanza kupata sura ya vazi la Taifa ili wadau 
walijadili na waamue ni vazi gani la Mtanzania ambalo litawakilisha 
Taifa kama nchi nyingine walivyomudu kuwa na vazi la Taifa.”
Aliongeza kuwa ili kufikia azma  Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezoiandae tamasha maalumu kwa ajili ya kuonesha aina tofauti za nguo ili kupata vazi la Taifa.
Kadhalika,
 Waziri Mkuu aliwaagiza waandaaji wa tamasha la Uridhi Festival 
wahakikishe kuanzia  mwakani kuwe na uratibu wa pamoja baina ya Tanzania
 Zanzibar na Tanzania Bara ili tamasha lifunguliwe upande mmoja na 
kufungwa upande mwingine wa Muungano.
Amesema
 kwa kufanya hivyo watakuwa wametoa  fursa kwa walio Zanzibar kujifunza 
na kuona utamaduni wa bara na wa bara kujifunza ya Zanzibar, hivyo 
itasaidia kudumisha  umoja wa kitaifa. “Hakikisheni ikiwa tamasha 
litafunguliwa Tanzania Bara basi lifungwe Zanzibar ili liweze kuwa na 
tija’’.
Katika hatua nyingine,Waziri Mkuu amesema Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020, inaitaka Serikali kuongeza msukumo katika kukuza utalii na kutangaza vivutio vyetu vya utalii vikiwemo utamaduni na malikale. 
“Mtakubaliana
 nami kwamba tunapaswa kuendeleza mila, tamaduni na desturi zetu kwani 
ndizo kichocheo muhimu cha uzalendo tulionao hususan katika suala zima 
la maadili. Vilevile, utamaduni ni zao la uhakika kwenye sekta ya utalii
 na ukarimu.” 
Amesema
 thamani ya utamaduni mara nyingi imekuwa ikionekana kwenye sekta 
nyingine kama elimu, afya, michezo, kilimo, viwanda na maendeleo ya 
jamii, ambapo alitoa rai kwaWizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo,
 wadau wote wa utalii hususani Sekta binafsi na wananchi kwa ujumla 
washirikiane katika kulinda, kutunza, kutangaza na kuendeleza vivutio 
vya utalii nchini.
“Lengo
 la Serikali ni kuongeza idadi ya watalii kutoka 1,102,026 mwaka 2015 
hadi 2,000,000 ifikapo mwaka 2020. Lengo hili linatekelezwa kwa 
kuwezesha sekta binafsi kuwekeza kwenye huduma ya miundombinu ya utalii 
na kuendelea kutangaza utalii ili kuwafikia watalii wengi zaidi.”  
Amesema Urithi
 Festival ni chachu ya kukuza, kulinda, kuimarisha nakutangaza utamaduni
 na malikale zetu na kuvigeuza kuwa zao la utalii. Tamasha hili 
litatuweka pamoja zaidi na kudumisha umoja, utaifa na uzalendo kwa nchi 
yetu.
Aidha,
 Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuikumbusha Wizara ya Maliasili na 
Utalii kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na
 Mkoa wa Dodoma kuanza maandalizi mara moja ya kutekeleza agizo la 
Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan la kutenga eneo mahususi ambalo 
litatumika kwa ajili ya Tamasha la Urithi kila mwaka kitaifa Mkoani 
Dodoma. 
“Napenda
 kutumia fursa hii na hasa nikizingatia maagizo ya Makamu wa Rais kuwapa
 changamoto Wizara ya Maliasili na Utalii na wadau wa utalii kuhakikisha
 kuwa kuanzia mwaka kesho (2019) tamasha hili linatambulika Kimataifa na
 kuwa moja ya kichocheo kikuu cha kukuza pato la Taifa litokanalo na 
utalii“
Amesema
 wakati wa uzinduzi wa tamasha hilo Septemba 15, 2018 jijini Dodoma, 
Makamu wa Rais, Mama Samia aliagiza kila Mkoa kutenga bajeti kwa ajili 
ya Tamasha la Urithi. “Napenda kutumia fursa hii kuwakumbusha tena Wakuu wa Mikoa kuanza maandalizi mapema.“
“Tamasha
 la Urithi sio tu linaenzi utamaduni na mila zetu, lakini ndio njia bora
 zaidi ya kurithisha vizazi vijavyo mila, desturi, tamaduni na historia 
yetu. Kwani yeyote yule ambaye haenzi utamaduni wake basi huyo ni 
mtumwa.“
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAMOSI, OKTOBA 10, 2018.
 
 
 
 

 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment