HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 09, 2019

TOTTENHAM YAIFUATA LIVERPOOL FAINALI MABINGWA ULAYA, YAITUPA NJE AJAX

Hii ni baada ya jana usiku kutoka nyuma kwa mabao 2-0 dhidi ya Ajax Amsterdam ya Uholanzi, kisha kushinda kwa mabao 3-2 na kuing’oa Ajax kwa sheria ya bao la ugenini. Pambano la kwanza baina yao, Ajax iliilaza Spurs 1-0. Iwapo Arsenal na Chelsea zitafuzu fainali ya Europa League leo usiku, basi England itakuwa nchi ya kwanza Ulaya kuingiza timu nne katia fainali mbili kubwa.
 Lucas Moura akiruka juu kushangilia moja ya mabao yake matatu aliyoifungia Tottenham. Picha na Daily Mail
 Lucas Moura wa Tottenham katikati akishangilia bao lake la tatu lililoipeleka timu yake fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya jana usiku
 Matthijs de Ligt wa Ajax akiruka juu kumzidi Dele Alli wa Tottenham na kuifungia bao la uongozi. Picha na Daily Mail
 Shangwe la ushindi na kutinga fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya. Picha na Daily Mail
 Wachezaji wa Tottenham wakishangilia ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Ajax, uliowapa nafasi ya kutinga fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya. Picha na Daily Mail.



AMSTERDAM, UHOLANZI

ENGLAND, huenda ikawa nchi ya kwanza Ulaya kuingiza timu nne katika fainali mbili za michuano mikubwa ngazi ya klabu barani humo, hii ni endapo Arsenal na Chelsea zitachanga vema karata zao katika mechi za marudiano nusu fainali Europa League leo usiku.

Tayari Tottenham Hotspur ya London, imeungana na Majogoo wa Jiji Liverpool katika fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya (UCL 2018/19), baada ya jana usiku kufanya ‘comeback ya kibabe,’ ikitoka nyuma kwa mabao 2-0 ya Ajax Amsterdam kipindi cha kwanza na kushinda 3-2.

Ulikuwa ni muendelezo wa maajabu ya soka, yaliyotokea saa 24 tu tangu Liverpool walipowababua FC Barcelona kwa mabao 4-0 na kupindua matokeo ya mechi yao ya kwanza wa mabao 3-0 dimbani Camp Nou, Barcelona nchini Hispania.
Katika nusu fainali ya pili jana, Tottenham, ikiwa na jeraha la kipigo cha bao 1-0 nyumbani, iliifuata Ajax Amsterdam ya Uholanzi kinyonge, hali iliyowafanya kuanza pambano kinyonge na kukubali kipigo cha mabao 2-0 ndani ya dakika 35, matokeo yaliyodumu hadi filimbi ya mapumziko.

Mabao ya Ajax katika dakika 45 za kwanza yalifungwa na Matthijs de Ligt mapema dakika ya tano, kabla ya Hakim Ziyech kuipa Ajax bao la pili dakika 30 baadaye, na kuibua shangwe kuu miongoni mwa mashabiki 53,285 kwenye dimba la Johan Cruiyff Arena, jijini Amsterdam.

Kipindi cha pili Totenham walikuja kivingine na Mbrazil Lucas Moura akafanya maajabu yake, baada ya kufunga mabao matatu ‘hat trick,’ na kuwapa Spurs ushindi wa mabao 3-2 na kuipeleka fainali yao ya kwanza kwa sheria ya bao la ugenini, kwani matokeo ya jumla yalikuwa ni 3-3.

Moura alifunga mabao yake katika dakika za 55 (pasi ya Dele Alli), dakika ya 59 (pasi ya Danny Rose) na kuhitimisha ushindi dakika ya 90+6 (pasi ya Alli na kuiwezesha Spurs kukata tiketiya kwenda Estadio Wanda Metropolitano, jijini Madrid, Hispania itakopigwa fainali Juni 1.

Macho na masikio ya Waingereza leo yanaelekezwa Hispania, ambako Arsenal walioshinda kwa mabao 3-1 katika mechi ya nyumbani Emirates, wanarudiana na Valencia kwenye viunga vya Mestalla, huku jijini London, Chelsea wakiwakaribisha Eintracht Frankfurt ya Ujerumani baada ya sare ya 1-1.

Wakati Arsenal watakuwa wakiwania ushindi ama sare ili kukata tiketi ya kwenda fainali mjini Baku, Azerbaijan, Chelsea wao watakuwa wakipigania sare tasa ama ushindi ili kuzalisha fainali ya Waingereza unayoweza kuiita ‘London Derby’ kutokana na upinzani wa klabu hizo za mji mmoja.

Iwapo Arsenal na Chelsea zitafanikiwa kutinga fainali ya Europa League, England itakuwa nchi ya kwanza kuingiza timu zote nne katika fainali mbili za michuano ya klabu Ulaya, lakini iwapo moja wapo itateleza, basi England inaweza kuingiza timu tatu katika fainali mbili.

·       Kumbukumbu zinaonyesha ya kuwa, mwaka 1980, Ujerumani iliingiza timu za Eintracht Frankfurt na Borussia Monchengladbach katika fainali ya UEFA Cup, huku timu nyingine ya nchi hiyo, Hamburg ikitinga fainali ya Europian Cup na kuumanana Nottingham Forest ya England.

·       Mwaka 1990, ni mwaka mwingine ambao nchi moja iliingiza timu tatu katika fainali mbili za michuano ya klabu Ulaya, baada ya Juventus na Fiorentina kuumana katika fainali ya Wataliano watupu ya UEFA Cup, huku AC Milan nayo ikitinga fainali Ligi ya Mabingwa.

·       Miaka minane baadaye (1998), Juventus ilitinga fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, huku klabu zingine mbili za Serie A, Inter Milan na Lazio, zikitinga na kuumana katika fainali ya UEFA Cup. 

·       Je England itaingiza timu nne fainali, au itaangukia kuwa nchi tatu Ulaya kuingiza timu tatu katika fainali mbili za michuano mikubwa barani Ulaya? Ni jambo la kusubiri na kuona na majibu yatapatikana leo usiku baada ya Arsenal na Chelsea kushuka viwanjani.

Kikosi cha Ajax katika mfumo  wa 4-2-3-1 na alama za ubora wao mchezoni: Onana 5; Mazraoui 6, Blind 6, De Ligt 7; Tagliafico 6; Schone 6.5 (Veltman 58, 6), De Jong 7; Ziyech 8.5, Van de Beek 6.5 (Magallan 90), Tadic 7.5; Dolberg 5 (Sinkgraven, 67, 6).

Kikosi cha Tottenham katika mfumo  wa 4-2-3-1 na alama za ubora wao mchezoni: Lloris 7; Trippier 5.5 (Lamela 81), Vertonghen 7, Alderweireld 6.5, Rose 7.5 (Davies 83); Sissoko 8, Wanyama 5 (Llorente 46, 7); Eriksen 6, Alli 7, Son 7; Moura 9.5.
Daily Mail

No comments:

Post a Comment

Pages