HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 26, 2019

Asasi za kiraia 300 zapendekeza kusitishwa kwa muswada wa mabadiliko ya sheria zinazohusu asasi

Baadhi ya viongozi wa Asasi za kiraia nchini wakizungumza na wanachama wao (hawapo pichani).
 

Na Janeth Jovin

ASASI 300 za Kiraia nchini zimependekeza kusitishwa kwa mchakato wa muswada wa mabadiliko ya sheria zinazohusu Asasi za kirai kwa kuwa umekuja kwa hati ya dharura na haukuwashirikisha wadau. 

Asasi hizo zimesema wadau wanapaswa washirikishwe vya kutosha katika mchakato wa muswada huo ili kupata maoni yao na  endapo muswada  huo ukipitishwa bila kuwashirikisha watakwenda kuupinga mahakamani kwani athari zake ni kubwa.

Akisoma tamko la asasi hizo jijini Dar es Salaam juzi, Mratibu wa Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini (THRDC), Onesmo Olengurumwa, alisema muswada huo uliopelekwa bungeni kama ukipitishwa na kuwa sheria basi utakwenda kuua asasi za kiraia zilizopo nchini.

Alisema muswada huo uliowasilishwa hivi karibuni bungeni  kwa hati ya dharura umezua sitofahamu na taharuki kwa azaki ambao ni walengwa wakuu kwenye muswada huo.

"Miongoni mwa sheria hizo ni sheria ya mashirikika yasiyo ya kiserikali ya mwaka 2002, sheria ya Jumuiya za kijamii, sheria ya mabaraza ya wadhamini na sheria ya makampuni ya mwaka 2002. Sheria hizi ni miongoni mwa sheria kuu zinazoongoza asasi za kiraia nchini," alisema.

Olengurumwa alisema uchambuzi walioufanya na asasi za kiraia zaidi ya 170 endapo muswada huo ukipitishwa utaleta changamoto nyingi katika utekelezaji na uendeshaji wa azaki.

Alisema miongoni mwa changamoto hizo ni kuminya kwa uhuru wa azaki nchini kinyume na katiba pamoja na mikataba mbalimbali ya kimataifa ambayo Tanzania imeridhia.

Alisema msajili amepewa mamlaka makubwa bila kudhibitiwa ya namna ya kusimamia azaki ikiwa ni pamoja kufuta usajili wa azaki pasipo kufuata utaratibu wa kisheria.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Usawa kwa Wasichana (EFG), Jane Magigita, alisema kutokana na changamoto walizoziona ni vizuri bunge likafanya maboresho na kufuta vipengele vinavyoathiri azaki za nchini.

"Tunawaomba wabunge kuusoma kwa umakini na kuuelewa muswada huu ili watakapokuwa ndani ya bunge watoe mapendekezo ya kurekebisha vipengele vyote vinavyoathiri azaki nchini," alisema

Magigita alisema wanaomba muswada huo uondolewe kwenye hati ya dharura na kushirikishwa katika hatua zote ikiwa ni pamoja na kukusanya maoni yao kutoka kwa wadau mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

Pages