HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 11, 2019

SADC KUSAIDIA SEKTA YA KILIMO NCHI WANACHAMA

NA SULEIMAN MSUYA

JUMUIYA ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), imesema inaendelea na mchakato wa kuunda Mfuko wa Kilimo wa Kanda kwa ajili ya kusaidia nchi wanachama katika sekta ya kilimo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Chakula, Kilimo na Maliasili (FANR) SADC,  Domingo's Gove wakati akielezea majukumu ya idara yake kwa waandishi wa habari jana jijiji Dar es Salaam.

Alisema sekta ya kilimo ni muhimu katika kuchochea maendeleo na uchumi wa nchi 16 za SADC hivyo ni wakati muafaka wa kuja na mfuko huo.

Alisema sekta ya kilimo inakabiliwa na changamoto mbalimbali kama mabadiliko ya tabia nchi, wadudu vamizi kama viwavijeshi ambapo njia ya kukabiliana navyo ni kuwepo na chombo rasmi kwa ajili hiyo.

"Katika kuhakikisha sekta ya kilimo inakuwa na tija kwa nchi wanachama tupo kwenye mchakato wa kuja na mfuko wa kilimo ambao utasaidia nchi zote," alisema.

Alisema mfuko huo utasaidia upatikanaji wa mbegu bora, mbolea, dawa  na kusaidia kilimo cha umwagiliaji kwa wakulima.

Gove alisema iwapo kila nchi itashiriki kikamilifu ni dhahiri sekta hiyo itachangia uchumi na maendeleo kwa kasi.

"Zipo mbegu zaidi ya 48 katika nchi wanachama za SADC ambazo wanazipa kipaumbele kulingana jiografia ya nchi husika," alisema.

Alisema mkakati wao ni kuwa na mbegu amabazo hazishambuliwi na wadudu vamizi kama viwavijeshi.

Mkurugenzi huyo alisema mfumo huo utasaidia utekelezaji wa vipaumbele vinne vya SADC katika sekta hiyo muhimu.

Alitaja vipaumbele vinavyosimamiwa na idara yake ni pamoja kukuza uzalishaji na ushindani katika sekta.

Pia alisema idara hiyo imejipanga kutafuta na kutangaza masoko, kuhamasisha sekta binafsi katika uwekezaji na kuongeza usalama wa chakula.

Aidha, mkurugenzi huyo alisema mipango na mikakati ambayo inatekelezwa na SADC itakuwa na tija iwapo itashabiahiana na Sera za nchi wanachama katika sekta husika.

Alisema sekta ya kilimo inaweza kuleta mapinduzi iwapo itashabihiana na uwepo wa viwanda, miundombinu, ulinzi na usalama na program maalum ambapo Tanzania imeonesha mfano.

Kwa upande mwingine Gove amezikumbusha nchi za SADC kutekeleza azimio walilokubaliana viongozi kwa  kutenga asilimia 10 katika Bajeti za nchi kuelekezwa Bajeti ya kilimo.

Alisema sekta hiyo ikipewa kipaumbele nchi na wananchi watafanikiwa kiuchumi na maendeleo

No comments:

Post a Comment

Pages