HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 22, 2019

RC KAGERA AWAWEKA NDANI WASIMAMIZI MIRADI YA UKARABATI SHULE KONGWE

Na Alodia Dominick, Bukoba

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Jenerali Marco Gaguti, amwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Revocatus Malimi, kuwaweka chini ya ulinzi wasimamizi watano wa miradi ya ukarabati wa Shule kongwe katika Manispaa ya Bukoba akiwemo Ofisa Ugavi na Manunuzi wa Manispaa kwa tuhuma za uzembe wa kusimamia na kasi ndogo ya ujenzi wa miradi katika shule hizo.

Mkuu wa mkoa Gaguti amechukua hatua hiyo Septemba 21, mwaka huu wakati wa ziara yake katika Manispaa ya Bukoba katika Shule kongwe za sekondari za Kahororo, Rugambwa, Kagemu na Bukoba ambazo kwa pamoja zilipewa fedha mwaka huu na serikali zaidi ya shilingi 2.5 bilioni kufanya ukarabati wa majengo ili kuzirejesha shule hizo katika hali nzuri lakini pamoja na  fedha hizo kuingizwa katika kila akaunti ya shule husika ukarabati umechukua muda mrefu na kuendelea kwa kusuasua na kupitiliza muda uliotolewa na Serikali kukamilika.

Mkuu huyo wa mkoa akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa baada ya kufika katika Shule ya Sekondari Kahororo na kutoridhishwa na ukarabati unaoendelea kwa kudorora pia kutoridhishwa na maelezo ya mkandarasi ambaye ni Festo Talimo wa kampuni ya Mzinga Holding amemwelekeza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera Revocatus Malimi kuwaweka chini ya ulinzi Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Marck Ogambage kwa uzembe wa usimamizi pamoja na Mhandisi Festo Talimo wa Mzinga kwa kufanya kazi kwa uzembe lakini pia ofisa Manunuzi wa Manispaa ya Bukoba Batreth Rwiguza kwa kufanya kizembe mchakato wa manunuzi ya vifaa vya ujenzi.

Wengine waliochukuliwa hatua kwa uzembe huo ni pamoja na Kaimu Mhandisi wa Manispaa ya Bukoba, George Geofrey,   kutosimamia ipasavyo ukarabati huo na kaimu mkuu wa shule ya sekondari Bukoba mwalimu Siasa Phocus pia amechukuliwa hatua kwa kuzembea kusimamia ukarabati wa shule hiyo huku zaidi ya 900 milioni zikiwa zimeishatumika kati ya Shilingi 1,481,701,194.33 bilioni zilizotolewa na Serikali kuhakikisha shule hiyo inarudi katika hali nzuri.

Richa ya wasimamizi hao kueleza changamoto mbalimbali zilizowakumba hazikuweza kusikilizwa na hivyo mkuu wa polisi mkoa wa Kagera kutii amri ya mkuu wa mkoa na kuwaweka chini ya ulinzi.

Shule ya Sekondari Kagemu ilipewa na Serikali Shilingi 152,000,000 milioni  tayari  muda wa ukarabati umeisha na zimelipwa 49,485,277.22 milioni, Shule ya Sekondari Kahororo ilipewa na Serikali shilingi  893,883,994 milioni kati ya hizo zimetumika shilingi 297,966,594.96 milioni muda wa ukarabati ukiwa umeisha bila kazi kukamilika na Shule ya Sekondari Rugambwa ilipewa shilingi 872,800,297 milioni na zilizotumika ni shilingi 275,125,889.25 milioni ambapo muda wa ukarabati ukiwa umeisha.

Pia mkuu huyo wa mkoa ametembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa barabara za kiwango cha rami kilomita tano ambao utagharimu shilingi 7.3 bilioni unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na kujengwa katika Manispaa hiyo ambao unatekelezwa na kampuni ya JASCO Building and Civil Engineering Contractors ya Jijini Mwanza.

Kwa upande wake Mhandisi wa Ujenzi katika Kampuni ya Jassie and Company Ltd  (JASCO), David Marko amezitaja changamoto zinazokumba ujenzi wa barabara hizo kuwa ni mvua inayonyesha kila asubuhi hivyo kukwamisha ujenzi huo na wakati mwingine kuharibu miundo mbinu hiyo maeneo ambayo yanakuwa yameishatengenezwa.

No comments:

Post a Comment

Pages