HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 28, 2019

TAFAYOCO yataja mambo manne ya kushiriki chaguzi

Na Suleiman Msuya

TAASISI isiyo ya Kiserikali ya Tanzania Feminist & Youth Change (TAFEYOCO), imetoa mapendekezo manne ya kuiwezesha jamii kushiriki uchaguzi; iwe kupiga au kupigiwa kura katika chaguzi zinazofanyika nchini mara kwa mara.
TAFEYOCO inakuja na mapendekezo hayo huku vyama vya siasa hasa vya upinzani vikilamikia mchakato wa uchaguzi wa Serikali Mitaa kuwa uligubikwa na figisu nyingi hali ambayo ilipelekea vyama nane kutangaza kujitoa.
Vyama ambavyo vilijitoa kushiriki uchaguzi huo uliofanyika Novemba 24 mwaka huu ni pamoja na Chadema, ACT-Wazalendo, CUF, UPDP, CCK, NCCR-Mageuzi, NLD na vingine.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa TAFEYOCO, Elvice Makumbo alitoa mapendekezo hayo ili iwe suluhu ya  chaguzi zingine zitakazofanyika kwa siku za usoni ikiwemo uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Alisema katika uchaguzi huo wa Serikali za Mitaa, wamegundua changamoto nyingi kuanzia kwa wagombea, wasimamizi na vyama vya siasa, hivyo wameona waje na mapendekezo yanayoweza kusaidia chaguzi zijazo  ziwe  rahisi.
Makumbo alisema taasisi yao inashauri Serikali ijikite katika utoaji wa elimu ya uraia ili wananchi wawe na ufahamu kuhusu masuala yote ya uchaguzi.
“Pendekezo la pili tunaomba asasi za kiraia zitumie nafasi yake kwa kuelimisha jamii kabla ya uchaguzi kufanyika na kushiriki katika uangalizi wa uchaguzi,” alisema.  
Mkurugenzi huyo alisema pendekezo la nne ni kuviomba vyama vya siasa kudumisha ushirikiano na mawasiliano kuanzia ngazi ya mitaa ili kuepusha migogoro kwenye vyama.
“Katika mchakato huu wa uchaguzi tumeona mapungufu mengi moja wapo ni vyama kukosa mawasiliano ya kiofisi ngazi ya chini hivyo inachangia baadhi ya maamuzi kugawanya wanachama,” alisema.
Alisema changamoto nyingine ambayo ilitokea ni wagombea kujaza fomu kwa mazoea akitolea mfano eneo la kuandika jina la chama wameandika kwa kifupi hali ambayo ni kinyume na sheria.
Mkurugenzi huyo alisema jamii imeonesha dhamira ya kushiriki siasa na chaguzi lakini kuna baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakitumia majukwaa ya siasa vibaya kwa kupotosha umma.
Aidha, Makumbo alitoa rai kwa vyama vya siasa kuacha tabia ya kususia uchaguzi kwasababu ndio njia ya kupata viongozi sahihi watakaosaidia kusukuma gurudumu la maendeleo.
Alisema TAFEYOCO ilishiriki kuangalia mchakato wa uchaguzi katika mkoa wa Dar es Salaam na Pwani ambapo katika maeneo yalifanya uchaguzi mwamko ulikuwa mzuri.

No comments:

Post a Comment

Pages