HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 30, 2019

MATIKO ATANGAZA MAZITO CHADEMA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2020

 Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Serengeti, Ester Matiko, akisisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi za Makao Makuu ya chama hicho Kanda, iliyopo Mjini Shinyanga. Matiko alizungumzia mikakati mbalimbali ya chama hicho, kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge mwaka 2020. (Picha na Sitta Tumma).


Na Sitta Tumma, Shinyanga

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Serengeti, kimetangaza mkakati wa kuanza kuzunguka maeneo yote kufanya siasa.

Kimesema Chadema kinaamini mwaka 2020 watashinda Urais na kuongoza nchi, hivyo wataunda Serikali tatu ya Tanganyika, Zanzibar na ya Shirikisho.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Serengeti, Ester Matiko, alipozungumza na waandishi wa habari mjini hapa, leo.

Alionya vyombo vya dola, akisema Chadema haitakubali kuvurugiwa tena mikutano yao.

"Msajili wa Vyama vya Siasa hadi sasa hajawahi kupokea lalamiko lolote lile la sisi kuzuiwa kufanya mikutano.
"Yaani kama vile hajui kuwa mikutano ambayo ipo kikatiba na kisheria imezuiwa. Safari hii hatukubali, hatukubali," Matiko alisema mbele ya wanahabari.

"Tuataka vyombo vya usalama visivuruge. Viheshimu Katiba, Sheria na haki za binadamu," alisisitiza.

"Sera yetu ni kuwa na Serikali tatu.  Ya Tanganyika, ya Zanzibar na ya Shirikisho (Muungano). Kila eneo litashughulikia maendeleo ya watu wake.

"Lakini, tutakuwa na mabunge kila kanda na bajeti zake. Huku Tanzania Bara Chadema tuna kanda nane, Zanzibar mbili," Mwenyekiti Matiko alisema.

Hata hivyo, alimuomba Rais Dk. John Magufuli, kuitangazia dunia kuufuta Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika mwaka huu.

Alisema uchaguzi huo unatakiwa upangwe kufanyika kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2020, iwapo Ikulu haikuingilia kuvurugwa kwake.

"Wasipofuta, Chadema tutatumia mawaziri kivuli wetu waliopo kisheria, kuwasemea wananchi kwenye Serikali za Mitaa," alisema Matiko.

Kiongozi huyo wa Chadema Kanda ya Serengeti, alisema iwapo Serikali inaamini imefanya vizuri miaka minne iliyopita, ingeacha uchaguzi wa Mitaa ufanyike, ili wapate mrejesho wa wanachi.

"Watanzania siyo wale wa leo wala jana. Walikuwa wanakwenda kuinyima kura CCM.

"Nawaomba Watanzania wote, Uchaguzi Mkuu ujao 2020, tukaiadabishe CCM kwa kuinyima kura kwenye sanduku la kura," Matiko alihimiza.

Matiko ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini, Mkoa wa Mara, alimshauri Rais Magufuli kutolipiga 'mnada' jengo la Ikulu lililopo Magogoni Dar es Salaam, kama ilivyowahi kukaririwa.

Badala yake ligeuzwe kuwa makumbusho ya kihistoria, litakalosaidia kuvutia watalii wengi kuzuru mjengoni pale.
"Mimi Rais sikumsikia akisema akihamia Dodoma pale atapapiga mnada. Kama ni kweli, namshauri apageuze kuwa makumbusho ya Taifa.

"Maana pale Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kakaa, Mzee Mwinyi kakaa, Mkapa kakaa, Kikwete kakaa pale na Rais Magufuli pia kakaa hapo," alisema.

Hata hivyo, Matiko aliyeanza kuzungumza na wanahabari saa 8:19 hadi 9:40 adhuhuri, alisema wanaamini licha ya kushinda Urais, Chadema itaongoza pia kwa wabunge na madiwani.

"Tunakwenda kudai tume huru ya uchaguzi. Tume hii itasababisha kura zetu za ushindi zilizopigwa zihesabiwe na kutangazwa kama zilivyo.

"Tumejipanga," alisema Matiko huku akiwabeza wabunge, madiwani na viongozi wengine waliohamia CCM kuwa huo ndiyo mwisho wa siasa zao, kwani huko hawatakuwa huru kuikosoa Serikali.

No comments:

Post a Comment

Pages