HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 08, 2020

Mtaka atia hamasa mbio za Mapinduzi Arusha

  TAMASHA la Mbio za Kuadhimisha Siku ya Mapinduzi ‘Mapinduzi Day Track Meet’ linatarajiwa kufanyika Januari 12 Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha likishirikisha mikoa mbalimbali.

Tamasha hilo limeandaliwa na Taasisi ya Gidabuday Sports Tourism Foundation (GSTF), kwa kushirikiana na Chama cha Riadha Mkoa wa Arusha (ARAA), na kuwezeshwa na kampuni ya Infinix.

Kwa mujibu wa Mtendaji Mkuu (CEO), wa GSTF, Eva Baltazar Gidabuday, tamasha hilo litakuwa na mbio za uwanjani ‘Track and Field’ sambamba na zile za kujifurahisha za Kilomita 10 ‘Fun Run’.

“Maandalizi yanakwenda vema na usajili wa washiriki unaendelea kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid kwa Sh. 5,000. Tayari baadhi ya wakimbiaji wakubwa wamesema watajitokeza kupima mida yao kama vile Alphonce Simbu, Gabriel Geay, Failuna Matanga na pia wanariadha kutoka mikoa ya jirani kama Kilimanjaro, Manyara, Tanga pia Zanzibar wametupigia kuelezea nia yao ya kutaka kushiriki na tunawakaribisha sana,” alisema Eva.
Eva, alizitaja mbio za uwanjani zitakazoshindaniwa siku hiyo ni mita 5,000, 800, 200, 400x4 Kupokezana Vijiti na Kuruka Chini kwa Wanaume na Wanawake.

Mtendaji huyo, alibainisha kuwa hakutakuwa na zawadi katika mbio hizo, lakini kwa upande wa uwanjani kuna hamasa imetolewa na Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Anthony Mtaka kwa washindi watatu wa kila tukio.

Alisema katika kuhamasisha zaidi mbio za uwanjani, Rais wa RT atatoa Sh. Kwa mshindi wa kwanza, Sh. 60,000 mshindi wa pili na Sh. 40,000 na mshindi wa tatu 20,000.

Aidha, Mtendaji huyo wa GSTF, alisema wako kwenye hatua nzuri klabu moja kutoka Colorado Marekani, kuwapa nafasi baadhi ya wanariadha watakaofanya vizuri kwenda kushiriki mbio mbalimbali za uwanjani zenye fursa ya kufuzu kwa Olimpiki Tokyo 2020.

Ikumbukwe, hivi karibuni Mtaka aliitaka mikoa mbalimbali kuandaa mbio za kupokezana ‘relays’ ili kupata wachezaji watakaunda timu ya Taifa kwa ajili ya kusaka viwango vya kushiriki Olimpiki Tokyo.

No comments:

Post a Comment

Pages