HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 16, 2020

UKUSANYAJI WA DAMU NCHINI WAONGEZEKA, JAMII YAHAMASIKA KUCHANGIA

 Mkurugenzi wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama, Dk. Magdelena Lyimo akizungumza na wanahabari (hawapo pichani) wakati wa ziara hiyo.
Mmoja wa wataalam akiwa kwenye shughuli za uhifadhi wa damu salama katika maabara ya kisasa.


NA ANDREW CHALE, DAR

MPANGO wa Taifa wa damu salama umebainisha kuwa jamii imehamasika kwa hali ya kutosha na kusaidia ongezeko kubwaa kujitokeza na kuchangia damu.

Imeelezwa kuwa, Chupa za damu 39379  zimekusanywa kwa mwaka 2018/2019 ukilinganisha na chupa 257557 mwaka 2017/2018  ambapo kwa ukusanyaji huo umefanya ukusanyaji kuongezeka kutoka asilimia 40 hadi 60 asilimia.

Hayo yameelezwa jana Jijini Dar es Salaam na Meneja  Mpango wa Taifa wa Damu Salama, Dkt. Magdelena Lyimo wakati wa kusoma taarifa yake kwa Maafisa Mawasiliano kutoka Wizara ya Afya pamoja na taasisi zake kwa ajili ya kutangaza maboresho ya Sekta hiyo hapa Nchini katika kampeni ya 'Tumeboresha Sekta ya Afya'.

Aidha, amebainisha kuwa licha ya kuongezeka kwa kiwango hicho, katika kuhakikisha wanaongeza huduma,  wako katika mpango wa kujenga kituo kikubwa cha damu Kanda ya Dodoma na tayari TSh. Bilioni 1.3 zimeshatengwa ili kufikia malengo makubwa zaidi ya ukusanyaji damu.

Akielezea namna wananchi wanavyohamasika, Dkt.  Lymo alisema jamii imekuwa na hamasa kubwa  ya kuchangia damu na mapokea yamekuwa makubwa karibu maeneo yote ya Nchi.

“Kazi zetu ni kuhakikisha uwepo wa  damu salama na ya kutosha na yenye ubora wa juu na ipatikane kwa wakati unaohitajika, tunahamasisha uchangiaji damu, tunatoa elimu, tunakusanya, tunapima, tunahifadhi na pia tunasambaza, pia tuna mwongozo wa uhamasishaji, ukusanyaji, usambazaji matumizi sahihi ya damu.

“Tuna vituo vya kanda saba, kuna Kanda ya Mashariki iko Mkoa Dar es Salaam, Kaskazini iko Kilimanjaro, Kanda ya Ziwa iko Mwanza, Kanda ya Magharibi iko Tabora, Kusini iko Mtwara na Kanda za Nyanda za Juu Kusini iko Mbeya.

“Kila kanda ina mikoa yake ambayo inahudumia. Pia kuna kanda za jeshi, hizi hazina mpaka wa kuhudumia,” alisema Dk. Lyimo.

Ambapo alibainisha kuwa, mpango huo wa damu salama unafanya kazi na hospitali za kibingwa ili kuweza kurahisisha upatikanaji wa damu kwa wagonjwa.

Aidha, Dkt. Lymo amesema Mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mine wameweza kufanya  ununuzi wa mashine 24 za maabara ambazo zimerahisisha shughuli za upimaji wa maambukizi katika damu na makundi ya damu kwa muda mfupi.

“Tumepata mashine mpya 24, kila kituo cha kanda kimepata mashine na gharama za mashine hizi ni Sh bilioni 13.2, kila kanda ina mashine nne ambapo mashine mbili ni za kupima maambukizi ya damu na mashine mbili za kupima makundi ya damu.

“Hizi za damu zina uwezo wa kupima sampuli 156 ndani ya saa mbili na ile ya kupima maambukizi inapima aina nne kama Ukimwi, homa ya ini B na C na kaswende. Hii ina uwezo wa kupima sampuli 100 ndani ya saa mbili, kwa sampuli 100 tunapata majibu 400 kutokana na kupima ugonjwa zaidi ya mmoja,” alisema Dk. Lyimo.

Hata hivyo alisema kuna mashine ya kisasa zaidi ambayo inapokea sampuli 600 na inatoa majibu ndani ya saa moja.

“Kwa mfumo wa nyuma, sampuli zilikuwa zinapimwa 88 ndani ya saa tatu au nne na unapata jibu moja, kwahiyo ililazimu wawepo watumishi wanne tofauti na sasa hata uwezekano wa kufanya makosa umepungua.

“Mpango wetu ni kuhakikisha tumeimarisha huduma na kanda zote saba zitafikia vigezo vya kitaifa na kimataifa,” alieleza Dkt. Lyimo.

Kutokana na uhitaji wa mazao yatokanayo na damu, alisema uhitaji wake utakuwa mkubwa hivyo uimarishwaji unaendelea wa upatikanaji wake.

“Tutaongeza matumizi ya mazao ya damu kama plate late, plasma na hizi zinahitajika kwa wagonjwa mfano kama saratani, figo na hata moyo, hivyo tunataka mgonjwa apate kitu anachokihitaji kwa wakati,” alisema Dkt.

No comments:

Post a Comment

Pages