HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 16, 2020

WAZIRI LUKUVI AZINDUA NMB NYANYUA MJENGO

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, akionyeshwa mchoro wa nyumba na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna, wakati wa hafla ya uzinduzi wa mikopo ya ujenzi wa nyumba uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kulia ni Ofisa Mkuu wa Wateja Wadogo, Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati, Filbert Mponzi. (Na Mpiga Picha Wetu).


NA SALUM MKANDEMBA

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, amezindua huduma mpya ya mikopo ya fedha za ujenzi ijulikanayo kama ‘NMB Nyanyua Mjengo’, inayotolewa na Benki ya NMB, huku akilitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), kushirikiana na benki hiyo.

Uzinduzi wa NMB Nyanyua Mjengo, huduma inayokwenda kuwa jawabu la changamoto za ujenzi wa ‘kuungaunga,’ ulifanyika Makao Makuu ya NMB, ambako Waziri Lukuvi aliitaja kama chachu katika upatikanaji wa makazi mapya 200,000 kwa kila mwaka, kulingana na mahitaji ya kitakwimu.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Waziri Lukuvi alibainisha kuwa, aina hiyo ya mikopo ni mwarobaini wa changamoto zote za upatikanaji wa nyumba bora na za kisasa miongoni mwa wananchi, na kwamba NHC inapaswa kuhamasisha wateja wao kuchangamkia fursa zinazokuja na NMB Nyanyua Mjengo.

“NHC inapaswa kushirikiana na NMB, kipato cha wananchi kwa sasa kiko chini, kuwakopesha nyumba zilizojengwa mahali pamoja ni kuwatisha mzigo, kwa hiyo wanapaswa wachukue wananchi wanaowasubirisha ujenzi kwa muda mrefu na kuwapeleka NMB, wapate mikopo na kujenga wenyewe,” alisema.

Waziri Lukuvi alisema takribani Hati za Viwanja milioni 1 zimetolewa na Wizara yake, lakini wamiliki wake wengi hawana uwezo wa ujenzi wa makazi katika viwanja hivyo na NMB inapaswa kuwafikia ili kuwafungulia fursa za mikopo yenye riba nafuu na ya muda mrefu.

Akizungumza kwa niaba ya NMB, Filbert Mponzi ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wakubwa na wa Kati wa benki hiyo, alisema wamejipanga kukidhi mahitaji ya mikopo ya fedha kwa wamiliki wa hati za viwanja kote nchini, lengo likiwa ni kufanikisha utimilifu wa ndoto za kumiliki makazi bora.

Mponzi alifafanua kuwa, mmiliki wa kiwanja anaweza kupata mkopo wa NMB Nyanyua Mjengo kuanzia Sh. Mil. 10 hadi 200, ambako mkopaji atarejesha katika kipindi cha hadi miaka 15 kwa riba nafuu, vigezo vya upataji mkopo vikiwa ni hati halisi na uwezo wa kifedha kufanya marejesho.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Ruth Zaipuna, alimpongeza Waziri Lukuvi na Serikali ya Awamu ya tano kwa ujumla kwa jitihada za kurasmisha makazi, kupima viwanja na kutoa Hati kwa wakati, yote yakilenga kuwawezesha wananchi kupata umiliki na makazi bora na ya kisasa.

Zaipuna aliwataka wananchi kuchangamkia huduma yao hiyo, kwani NMB wamejipanga na wana fungu la kutosha linalofikia kiasi cha Sh. Bil. 23 zilizotengwa kufanikisha mikopo ya NMB Nyanyua Mjengo na kwamba kiasi hicho kinaweza kuongezeka kulingana na mahitaji ya wateja. 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mikopo ya Nyumba ya Tanzania Mortgage Refinance (TMRC), Oscar Mgaya, aliipongeza NMB kwa ubunifu uliozaa huduma hiyo ya mikopo, aliyoiita suluhu ya changamoto za ujenzi na nguvu ya ziada kwa wakopaji.

Mgaya aliongeza kuwa, wao kwa upande wao kama wawezeshaji, wamevutiwa na kuweka utayari wa kufanikisha hilo kwa kuiongezea nguvu NMB katika kupata fungu la kutosha kutoa mikopo ya muda mrefu, ili kurahisisha mpango wa ukopeshaji kwa wananchi wa kada zote.

No comments:

Post a Comment

Pages