NA SULEIMAN MSUYA
OFISA
Sera na Majadiliano wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania
(MJUMITA), Elida Fundi amesema iwapo vijiji vyenye misitu ya asili
vitatumia rasilimali hiyo kwa njia endelevu vitapata maendeleo kwa
haraka.
Fundi amesema
hayo wakati akizungumza na wananchi wa vijiji vya Mtawatawa na Darajani
wilayani Liwale mkoani Lindi ambapo alitembelea akiambatana na waandishi
wa habari kutoka vyombo mbalimbali.
Amesema
misitu ni bidhaa ambayo ina fursa nyingi kama wanavijiji watapata elimu
kuhusu faida zilizopo hasa wanapotumia kwa njia endelevu.
Ofisa
huyo amesema MJUMITA kwa kushirikiana na Shirika la Kuhifadhi Misitu ya
Asili Tanzania (TFCG) wamekuwa wakiibua miradi mbalimbali ambayo
inasaidia wanavijiji kuona fursa zilizopo kwenye misitu na mwitikio ni
mzuri.
"MJUMITA na TFCG
tunatambua fursa zilizopo kwenye misitu ndio maana kila kukicha tunabuni
miradi kama Mradi wa Kuleta Mageuzi katika Sekta ya Mkaa (TTCS) ambao
umefikia vijiji zaidi ya 30 katika wilaya ya Kilosa, Mvomero na Morogoro
mkoani Morogoro.
Pia kwa
sasa tunatekeleza Mradi wa Kuhifadhi Misitu kwa Kuwezesha Biashara
Endeley ya Misitu (CoFoREST) chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo
la Uswisi (SDC) imeonesha matokeo chanya ya kimaendeleo, uchumi na
jamii," amesema.
Fundi amesema vijiji venye kutekeleza Mpango wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu (USMJ) umechochea maendeleo na kuongeza uhifadhi.
Amesema vijiji vimeweza kutekeleza miradi mikubwa kwa muda mchache tofauti na awali ambapo miradi mingi imekuwa ikisuasua.
Ofisa
huyo amevitaka vijiji vingine vyenye misitu ya asili kuitumia kwa dhana
ya USMJ ili kuweza kuchochea maendeleo yao na ya vijiji.
"USMJ
imepunguza mzigo mkubwa kwani misitu imesaidia kutekelezwa kwa miradi
ya shule, zahanati, maji, elimu, afya na mingine mingi huku uhifadhi
ukiongezeka," amesema.
Katibu
Tawala wa Wilaya ya Liwale Rajabu Kambangwa amesema wilaya hiyo
inatambua mchango wa sekta ya misitu hivyo wataendelea kuunga mkono
juhudi zinazofanywa mashirika kama MJUMITA, TFCG na mengine.
Kambangwa
amesema misitu ni moja ya chanzo cha uhakika cha mapato wilayani ambapo
kwa mwaka wanakusanya zaidi ya shilingi bilioni 2 zinaoelekezwa kwa
miradi ya maendeleo.
"Sisi
tunakusanya kodi kupitia vyanzo mbalimbali lakini kusema ukweli sekta
ya misitu imekuwa na mchango mkubwa wa maendeleo," amesema
DAS
huyo amesema wamekuwa wakisisitiza wanavijiji kutunza mazingira ili
kuhakikisha wanaweza kukabiliana na mabadili ya tabia nchi.
Amesema wanaendelea na utoaji elimu kwa wananchi wa vijiji vyote ambavyo rasilimali mksutuninakuwa rasmi.
Katibu
Tawala huyo amesema ushirikiano ndio mbinu pekeee ambayo inaweza
kuchochea maendeleo hivyo kuyataka mashirika mengine kujitokeza na
kuwekeza kwenye sekta hiyo muhimu.
Amewataka
wananchi wa wilaya ya Liwale ambao vijiji vyao vina Vasili misitu ya
asili kuitumia vizuri ili kuweza kuondoa changamoto za uhaba wa
madarasa, nyumba za walimu, vituo vya afya na huduma nyingine muhimu.
Baadhi
ya mwananchi wa vijiji vya Mtawatawa na Darajani wamesema fursa
wanazozipata kupitia USMJ ni nyingi hivyo kuahidi kuungamkono miradi ya
MJUMITA na TFCG.
No comments:
Post a Comment