HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 12, 2022

BENKI YA CRDB YATOA MSAADA WA TAULO ZA KIKE KWA WANAFUNZI RUANGWA

 


Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Mkoani Lindi, Upendo Mfilinge akikabidhi msaada wa taulo za kike kwa Mwanafunzi wa Darasa la Sita wa Shule ya Msingi Likunja Shadia Mbochele wakati wafanyakazi wa benki hiyo tawi la Ruangwa walipoadhimisha siku ya mwanamke duniani inayofanyika Tarehe 8, Machi kila mwaka. Msaada huo ukiwa ni utaratibu wa Benki hiyo kujitolea kusaidia jamii yenye uhitaji. Hafla ya kukabidhi msaada huo imefanyika katika Shule ya Msingi Likunja hivi karibuni.


Msimamizi wa Sheria na Miongozo wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Faraja Haule akikabidhi moja ya msaada wa taulo za kike kwa Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Ruangwa wakati wafanyakazi wa benki hiyo tawi la Ruangwa walipoadhimisha siku ya mwanamke duniani inayofanyika Tarehe 8, Machi kila mwaka.


Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Mkoani Lindi, Upendo Mfilinge akikabidhi moja ya msaada wa taulo za kike kwa Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Ruangwa wakati wafanyakazi wa benki hiyo tawi la Ruangwa walipoadhimisha siku ya mwanamke duniani inayofanyika Tarehe 8, Machi kila mwaka.

 

Afisa Uhusiano wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Mkoani Lindi, Francis akikabidhi msaada wa taulo za kike kwa Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Ruangwa Zainabu Madina  wakati wafanyakazi wa benki hiyo tawi la Ruangwa walipoadhimisha siku ya mwanamke duniani inayofanyika Tarehe 8, Machi kila mwaka. Msaada huo ukiwa ni utaratibu wa Benki hiyo kujitolea kusaidia jamii yenye uhitaji. Hafla ya kukabidhi msaada huo imefanyika katika Shule ya Msingi Likunja hivi karibuni.

 

Na Mwandishi Wetu, Ruangwa

 

BENKI ya CRDB kupitia Wafanyakazi wa Benki hiyo Tawi la Ruangwa mkoani Lindi imetoa msaada wa taulo za kike katika kuazimisha siku ya Wanawake Duniani ambayo huazimishwa tarehe 8 ya mwezi wa tatu katika Shule ya Sekondari Ruangwa  na Shule ya Msingi Likunja za wilayani humo.

 

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Mkoani Lindi, Upendo Mfilinge alisema wametoa msaada huo ili kuwasaidia watoto wa kike kusoma kwenye mazingira salama hali itakayowasaidia kuongeza bidii kwenye masomo yao.

 

"UPATIKANAJI wa Taulo za Kike ni muhimu kwa maudhurio ya mtoto wa kike shuleni  katika kuwawezesha wanafunzi wa kike kuhudhuria shule kikamilifu na kupata haki msingi ya elimu sawa na vijana wa kiume," alisema Bi Upendo.

 

Meneja huyo alisema kwamba ndani ya benki yao wamefanya hivyo wakiamini kuwa ukimuwezesha mwanamke umeiwezesha jamii na hivyo ndio moja ya siri kubwa ya mafanikio kwenye benki hiyo.

 

Nae Mwalimu wa Afya wa Shule ya Msingi Likunja, Happiness Amlima akizungumza wakati wa hafla ya kupokea msaada wa uzinduzi wa Taulo za Kike shuleni hapo alisema wanafunzi wengi wa kike shuleni hapo huvaa vitambaa ambavyo sio salama kwa afya zao wawapo hedhini.

 

Pamoja na jitihada zinazofanywa na wadau mbalimbali ikiwemo serikali bado mahudhuria ya watoto wa kike mashuleni hayaridhishi na hivyo kupelekea kutokufanya vizuri katika masomo yao, changamoto hiyo kwa kiasi kubwa imechangia watoto wengi wa kike wakati wanapoingia kwenye kipindi chao cha hedhi kutokuwa na uwezo wa kuwa na taulo bora za kike nakuwalazimu kukaa nyumbani na kushindwa kuja shuleni mpaka watakapomaliza." alisema Mwalimu Happiness.

 

Awali Mwalimu Mkuu Msaidizi wa  Shule ya Sekondari Ruangwa Mwisio Tuyanje amewashukuru wafanyakazi wa benki ya CRDB tawi la Ruangwa kwa kuitembelea shule hiyo na kutoa msaada huo wakati ikiadhimisha siku ya mwanamke duniani inayofanyika Tarehe 8, Machi kila mwaka.

 

Kwa kweli niwashukuru sana na kuwapongeza uongozi wa Benki ya CRDB tawi la Ruangwa kwa kutambua umuhimu wa huduma hii kwa mtoto wa kike kwenye shule zetu, nimefurahishwa sana kwa kujali na kutoa mahitaji haya ambayo ni muhimu kwa vijana wetu wa kike”Alisema Mwalimu Tuyanje.

 

Naye Msimamizi wa Sheria na Miongozo wa Benki ya CRDB Tawi la Ruangwa Faraja Haule amezikumbusha taasisi mbalimbali kushiriki kusaidia shule ambazo zipo pembezoni zinazokosa fursa ya kupata misaada ya mara kwa mara ukifananisha na zile zilizopo mijini.

 

"Mara nyingi taasisi nyingi hushiriki kutoa misaada kwa shule zilizo mijini na kuzisahau shule zilizopo vijijini, ambazo wanafunzi wake wanatoka kwenye mazingira duni wenye uhitaji," alisema Bi Faraja Haule.



No comments:

Post a Comment

Pages