HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 13, 2022

RUWASA yatumia Sh. milioni 970 kupeleka maji Daraja Mbili, Kazamoyo


Kaimu Meneja wa RUWASA wilaya ya Tunduru, Mhandisi Silvia Ndimbo, akitoa maelekezo kwa Mkandarasi wa Kampuni ya Ujenzi ya Civito, Mhandisi Stanley Mlelwa kuhusu ujenzi wa tenki la maji la Daraja Mbili wilayani hapo.

Baadhi ya mambomba ambayo yamesambazwa katika vijiji vya Daraja Mbili na Kazamoyo wilayani Tunduru mkoani Ruvuma.
 
Na Selemani Msuya, Tunduru

WAKALA wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma imetumia zaidi ya Sh.milioni 974.8 kumaliza kero ya maji katika vijiji vya Kazamoyo na Daraja Mbili ifikapo mwishoni mwa mwezi Mei, mwaka huu.

Hayo yamesemwa na Kaimu Meneja wa Ruwasa wilayani Tunduru, Mhanmdisi Silvia Ndimbo wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii ambaye alitembelea miradi ya maji inayotekelezwa kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya Uviko-19. 

Miradi hiyo ya maji inatekelezwa kupitia fedha za mkopo usio na riba kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Sh. trilioni 1.3 zilizokopwa na Serikali ya Tanzania.

Mhandisi Ndimbo amesema Tunduru imepata miradi miwili ambayo inatekelezwa katika majimbo mawili ya Tunduru Kusini na Kaskazini kwa fedha za ustawi.

Kaimu meneja huyo amesema miradi hiyo itagharimu zaidi ya Sh. milioni 974 ambapo Mradi wa Maji Kazamoyo unagharimu Sh.milioni 476.5 na Daraja Mbili Sh.milioni 498.3 ambapo kazi zote zipo katika hatua nzuri.

“Kazi ambazo zinatekelezwa ni uchimbaji wa mitaro, ulazaji wa mabomba ambapo hadi sasa kilomita 16 kati 18 bomba limesambazwa, ujenzi wa vituo saba, tanki na nyumba ya mitambo,” amesema.

Kaimu meneja huyo amesema miradi hiyo inayotekelezwa na Kampuni ya Ukandarasi Civito itaongeza asilimia ya upatikanaji wa maji wilaya hiyo hadi kufikia asilimia 68 na matarajio yao kufikia asilimia 74 ya upatikaji wa maji mwisho wa mwaka huu.

“Ipo miradi ya Mtuwesi, Senene, Basiburu, Kazamoyo, ufungaji wa pampu katika vijiji 20 na uchimbaji wa visima 18, ambapo matarajio yetu ni ifikapo 2025 tutakuwa tumefikia asilimia 85,” amesema.

Amesema Tunduru ina changamoto kubwa ya vyanzo vya maji na kwamba asilimia kubwa ya maji yanayotumika yanatokana na visima, hivyo wanaomba Serikali Iendelee kutoa fedha za miradi ya maji.

Mhandisi Ndimbo amesema anaishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuipatia RUWASA fedha za miradi ya maji hali ambayo itafanikisha kauli mbiu yao ya maji bombani hivyo kumtua ndoa mama kichwani.

Kwa upande wake Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Rebman Ganshonga amesema watahakikisha wanashirikiana na mameneja wa RUWASA wilaya kufanikisha lengo la upatikanaji maji vijiji kwa asilimia 85 ifikapo 2025.

Mhandisi Ganshonga amesema RUWASA inatambua umuhimu wa upatikanaji wa maji safi na salama, hivyo fedha inayopatikana inatumika kama ilivyopangwa, ili kuweza kumtua ndoo mama kichwani.

"Sisi RUWASA tunaposema kumtua mama ndoo kichwani tunamaanisha maji yatoke bombani na hili limetimia kwa asilimia nzuri,"amesema

Aidha, Mhandisi Ganshonga amesema katika kuhakikisha maji yanapatikana kwa uhakika wanashirikiana na wadau wote kutunza mazingira.

Naye Mkandarasi kutoka Kampuni ya Civito, Mhandisi Stanley Mlelwa amesema miradi hiyo itakamilika kwa wakati ili kuhakikisha wananchi wa vijiji vya Kazamoyo na Daraja Mbili ambayo hawajawahi kutumia maji ya bomba tangu kupata uhuru wanayapata. 

"Miradi hii miwili tunaitekeleza kwa ufanisi mkubwa ili kuhakikisha wananchi wanapata maji kwa wakati,"amesema.

No comments:

Post a Comment

Pages