HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 27, 2022

WHO: Idadi ya Wazee kuwa kubwa kuliko watoto chini ya miaka 15


 

 Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani –WHO Dr Zabulon Yoti akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam kuhusu kuelekea Siku ya Wazee Duniani itakayoadhimishwa Oktoba Mosi mwaka huu.

 
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Kimataifa la HelpAge Joseph Mbasha akizungumza na wanahabari jijini Dar es salaam kuhusu kuelekea siku ya wazee Duniani.
 
 
Na Hussein Ndubikile, Dar es Salaam

Imeelezwa kuwa kwa kipindi cha sasa idadi ya wazee ni kubwa kuliko watoto chini ya miaka 15 na mpaka kufika mwaka 2050 karibu asilimia 21 ya watu wote duniani watakuwa ni wazee.

Hayo yamebainishwa leo jijini Dar es salaam katika Mkutano wa Shirika la Afya Duniani -WHO na waandishi wa habari kuhusu kuelekea siku ya wazee Duniani ambapo inatarajiwa kuadhimishwa Oktoba mosi mwaka huu

Akizungumza katika kikao hicho Mwakilishi Mkazi wa Shirika hilo Dkt. Zabulon Yoti amesema malengo yao ni kuhakisha wanaendeleza jitihada za kuwasaidia wazee hasa katika mapambano ya UVIKO -19.

Kwa upande wake,Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Kimataifa la HelpAge, Joseph Mbasha ameitaka jamii kuepukana na dhana ya kuwatuhumu wazee kuwa na imani za kishirikina kwani kufanya hivyo ni kuwaondolea utu wao.

‘Jambo ambalo limekuwa likiniumiza tumekuwa tukitumia nafasi hii kwamba huyu mzee ni mshirikina (mchawi) jambo ambalo linasababisha anapigwa na wananchi na kuuawa hivyo ni vyema jamii tukaondokana na dhana hiyo ya kuwadidimiza wazee’amesema Mbasha

Amesisitiza kuwa changamoto nyingine inayowakumba wazee ni watu kutumia kauli ya kuwa wazee wamepitwa na wakati katika ufanyaji wa shughuli mbalimbali za kimaendeleo ilhali wana nguvu ya kufanya kazi.

Nae, Mtaalamu wa Chanjo wa WHO, Dkt Willium Mwengee amesema Shirika la Afya Duniani liliamua wazee walindwe dhidi ya maradhi huku Afisa Program wa Dawa na Vifaa Tiba Rose Shija akisema pia shirika hilo linawasaidia wazee kupata vifaa visaidizi.

Hata hivyo kwa mujibu wa takwimu imeelezwa katika nchi zinazoendelea asilimia 20 ya wazee wapo kwenye mifumo ya Hifadhi ya Jamii huku kwa Tanzania ikiwa ni asilimia saba pekee.

No comments:

Post a Comment

Pages