HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 21, 2022

WASHIRIKI 3,000 WAJISAJILI NMB MARATHON, KITS HADHARANI

 Afisa Mkuu Raslimali watu wa Benki ya NMB, Emmanuel Akonaay akizungumza wakati wa kutambulisha Jezi na Medali zitakzotumika kwenye NMB Marathon, kutoka kushoto ni Nahodha msaidizi wa NMB Joging Club, Stella Moto, Mkuu wa Idara ya Bima, Martine Masawe na Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya NMB Marathon Mercy Nyange.
Raslimali watu wa Benki ya NMB, Emmanuel Akonnay, Mkuu wa Idara ya  Bima Martine Massawe, Mwenyekiti Kamati ya Maaandalizi ya NMB Marathon, Mercy Nyange (kulia) na  kushoto ni Nahodha msaidizi wa NMB Joging Club Stella  Motto wakionyesha jezi na Medali zitazotumika kwenye mbio za NMB Marathon zitakayofanyika tarehe moja mwezi wa kumi katika viwanja vya Leaders Club Dar es Salaam.

LICHA ya washiriki zaidi ya 3,000 kujisajili kushiriki Mbio za Hisani za NMB Marathon 2022, Benki ya NMB imeeleza sababu za kusogezwa mbele kwa mbio hizo, huku ikitambulisha medali na jezi zitakazovaliwa, pamoja na kumthibitisha Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuwa Mgeni Rasmi.

NMB Marathon zitafanyika Oktoba Mosi badala ya Septemba 24 kama ilivyokuwa imepangwa awali, zikianzia na kumalizikia katika Viwanja vya Leaders Cub, Kinondoni jijini Dar es Salaam, lengo likiwa kukusanya Sh. Milioni 600 za kusaidia matibabu ya kinamama wenye Fistula kwenye Hospitali ya CCBRT.

Akizungumza wakati wa utambulisho wa fulana na medali hizo, Afisa Mkuu wa Rasirimali Watu wa Benki ya NMB, Emmanuel Akonaay, alisema hadi jana asubuhi zaidi ya washiriki 3000 wamejisajili na kuwa vifaa ‘kits’ vilivyoandaliwa kwa wakimbiaji hao ni vya ubora wa kimataifa.

Alibainisha kuwa, katika kujiweka sawa kwa mbio hizo, NMB ilifanya bonanza la NMB na Wabunge wiki jana, ambalo wamelitumia kama maandalizi, ushawishi na mialiko kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ili waweze kuwa sehemu ya washiriki wa mbio hizo.

“Tunaamini wabunge hao ni miongoni mwa watakaonufaika na uamuzi huu wa kusogeza mbele, ambao umetokana na maombi ya wengi miongoni mwa Watanzania, kututaka tusogeze ili waweze kushirikiana nasi katika tukio hili, linaloenda kurejesha tabasamu kwa kinamama wenye Fistula.

“Kwa hiyo usajili unaendelea Mbezi Beach, Juliana Pub iliyopo Mtana Bar pale Kanisa la St. Peters, Mlimani City na kwenye tovuti ya marathon.nmbbank.co.tz. Watanzania wazidi kujisajili na waliofanya hivyo tayari, wafike kuanzia kesho (leo) Mlimani City kuchukua ‘kits’ zao,” alifafanua Akonaay.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya NMB Marathon, Mercy Nyange, alibainisha kwamba benki yake inashukuru kupata wadhamini wengi waliojitokeza kudhamini mbio hizo ili kuunga mkono jitihada za kulikomboa kundi la kinamama, wanaokabiliwa na changamoto hiyo.

Mercy aliwaomba Watanzania walioomba kuongezwa kwa muda wa usajili kujitokeza na kwamba udhamini mnono kutoka Sanlam, UAP, Toyota na kampuni nyinginezo, unawahakikishia zawadi nzuri kwa washindi wa kwanza hadi wa 10 kategori zote za kilomita 5, 10 na 21, pamoja na mbio za watoto.

“Niweke msisitizo tu, kama ilivyosemwa washiriki zaidi ya 3,000 wamejisajili hadi sasa, kwahiyo fursa hii iliyoombwa itumiwe vizuri na watu wajitokeze kujisajili katika maeneo yaliyotajwa hapo juu,” alisisitiza Mercy.

 

No comments:

Post a Comment

Pages