Mwenyekiti wa Bodi ya Mpito ya Tanzania Breweries PLC (TBL) (kushoto), Ami Mpungwe, Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle Kilpin (katikati), akizungumza na wanahisa wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa TBL na kulia ni Mkurugenzi wa Fedha wa TBL, Avito Swai, ambapo wanahisa waliidhinisha taarifa za fedha za kampuni zilizokaguliwa kwa mwaka wa 2025 kufuatia mwaka wa ukuaji wenye faida.
Dar es Salaam, Tanzania –
Alhamisi, tarehe 2 Julai 2026: Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL Plc)
leo imefanya Mkutano Mkuu wa 53 wa Wanahisa katika Kituo cha Kimataifa cha
Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, huku wanahisa wengine
wakishiriki kupitia mfumo wa mkutano wa mtandaoni.
Mkutano huo uliwapa wanahisa fursa
ya kupitia utendaji wa kampuni kwa mwaka 2025, kuidhinisha masuala muhimu ya
utawala bora wa kampuni na kujadiliana na Bodi ya Wakurugenzi pamoja na
Menejimenti kuhusu mwelekeo wa kampuni.
Katika mkutano huo, wanahisa
walipitisha kumbukumbu za Mkutano Mkuu wa 52 wa Wanahisa, wakapitisha Ripoti ya
Wakurugenzi, Ripoti ya Wakaguzi wa Hesabu na taarifa za fedha zilizokaguliwa
kwa mwaka ulioishia tarehe 31 Desemba 2025, pamoja na kuthibitisha mgao wa muda
uliolipwa kwa mwaka huo.
Wanahisa pia waliidhinisha uteuzi
wa kampuni ya PricewaterhouseCoopers kuwa wakaguzi wa hesabu wa nje kwa mwaka
wa fedha unaoishia tarehe 31 Desemba 2026.
TBL iliripoti mwaka wenye ukuaji
mkubwa wa faida ambapo mapato yaliongezeka kwa asilimia 13 na faida ya
uendeshaji ikaongezeka kwa asilimia 35. Matokeo hayo yalichangiwa na ongezeko
la mahitaji ya bia na vileo vikali, usimamizi madhubuti wa gharama, uwekezaji
endelevu katika chapa pamoja na maboresho katika mfumo wa usambazaji wa bidhaa
sokoni.
Balozi Ami R. Mpungwe,
Mwenyekiti wa Muda wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanzania Breweries PLC, alisema
kuwa Mkutano Mkuu wa Wanahisa umeendelea kuthibitisha dhamira ya kampuni ya
kuzingatia utawala bora, kuimarisha imani ya wanahisa na kuendelea kujenga
thamani ya muda mrefu.
"Mkutano Mkuu wa Wanahisa
unabaki kuwa jukwaa muhimu la uwajibikaji kwa TBL. Unawapa wanahisa taswira ya
wazi kuhusu utendaji wa kampuni, utawala wake na mwelekeo wake wa baadaye. Bodi
itaendelea kutoa usimamizi madhubuti, kulinda maslahi ya wanahisa na kuunga
mkono Menejimenti huku kampuni ikiendelea kukua kwa uwajibikaji na kuchangia
maendeleo ya uchumi wa Tanzania."
Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle
N. Kilpin, alisema kuwa matokeo ya mwaka 2025 yanaonesha nguvu ya
chapa za kampuni, wafanyakazi wake, wateja na wadau wote katika mnyororo wa
thamani.
"Matokeo yetu ya mwaka
2025 yamechochewa na uimara wa chapa zetu, utekelezaji wenye nidhamu pamoja na
imani ya watumiaji wetu, wateja na wanahisa. Tutaendelea kuwekeza katika chapa
zinazopendwa na watumiaji, kuimarisha mifumo yetu ya kidijitali, kuongeza
matumizi ya malighafi za ndani na kuboresha ufanisi wa shughuli zetu. Lengo
letu ni kukua kwa uwajibikaji huku tukitengeneza thamani kwa wanahisa wetu na
mfumo mzima unaoiunga mkono TBL nchini Tanzania."
Mbali na mafanikio ya kifedha, TBL
iliendelea kuimarisha mchango wake katika mnyororo wa thamani wa ndani. Mwaka
2025 ulikuwa mwaka wa kwanza kamili wa uendeshaji wa Kiwanda cha Kimea cha
Kilimanjaro, ambacho kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha tani 8,000 za kimea kwa
mwaka na hivyo kuongeza matumizi ya shayiri inayolimwa nchini.
Kampuni pia iliendelea kupanua
mfumo wa kidijitali wa kuagiza bidhaa, kuimarisha ushirikiano na wauzaji wa
rejareja pamoja na kuwaunga mkono wakulima wadogo wa shayiri na mtama.
Uendelevu uliendelea kuwa sehemu
muhimu ya mkakati wa muda mrefu wa TBL. Mwaka 2025, asilimia 92 ya vifungashio
vya kampuni vilikuwa vinaweza kurejeshwa au vilitengenezwa kwa kiwango kikubwa
kutokana na malighafi zilizorejelewa. Aidha, matumizi ya maji yaliendelea kuwa
wastani wa hekta lita 2.55 kwa kila hekta lita moja ya uzalishaji. Kampuni pia
iliendelea kuhamasisha matumizi yenye uwajibikaji ya bidhaa zake na kusaidia
maendeleo ya wafanyabiashara wa rejareja nchini kote.
Bodi ya Wakurugenzi pamoja na
Menejimenti waliwashukuru wanahisa kwa kuendelea kuiamini kampuni na kusisitiza
dhamira ya TBL ya kuendelea kukuza biashara, kuimarisha chapa zake, kutekeleza
mikakati yake kwa nidhamu na kujenga thamani endelevu.
Kadri TBL inavyoadhimisha Mkutano Mkuu wake wa 53 wa Wanahisa, kampuni inaendelea kujenga juu ya historia yake ndefu ya ushirikishwaji wa wanahisa, ukuaji wa chapa zake na mchango wake katika uchumi wa Tanzania. Dhamira yake inaendelea kuwa kukuza biashara kwa uwajibikaji, kuwekeza katika chapa zinazoaminika na kuendelea kutengeneza thamani kwa wanahisa, wateja, wafanyakazi, wasambazaji, wauzaji wa rejareja, wakulima na jamii nchini kote.









No comments:
Post a Comment