HABARI MSETO (HEADER)


October 29, 2022

Ugumba; Tatizo lenye tafsiri tata kiimani na kijamii-1

Wataalamu wa wanawake na uzazi, wakiendelea na huduma. (Picha na Mtandao).


NA CHRISTINA MWAKANGALE
 

NI ndoto ya kila mwanamke kwamba afikapo umri wa utu uzima iwe ameolewa au hajaolewa, kupata mtoto, ingawa matarajio hayo kwa wenye imani tofauti ikiwamo dini ni kudra za mwenyezi Mungu. 

Pamoja na matarajio hayo, ugumba hukatiza ndoto za wanawake wengi. Ugumba ni tatizo la kushindwa kushika mimba kwa njia ya kibaolojia na linatibika.

Kadhalika mabingwa wa kinamama na uzazi, watatafsiri ugumba ni hali ya mwanamke kushindwa kupata ujauzito kwa kipindi cha mwaka mmoja, ilhali upo kwenye ndoa au mahusiano na hatumii njia yeyote kuzuia mimba.

Pamoja na hayo, kukua kwa teknolojia duniani kumetafsiri tofauti hali hiyo, na kurudisha faraja kwa wanawake waliosubiri ujauzito muda mrefu, kwa njia ya kiteknolojia, ikiwamo huduma ya kupandikiza mimba (In vitro Fertilization-IVF).

Veneranda Alfred (48), anajihisi ndoto hiyo haijatimia kwake hadi sasa, licha ya kuwashirikisha viongozi wa dini wa kanisa anakosali ya kile kinachomsibu kwa muda mrefu, akiwataka wamfanyie maombi, apate mtoto.

Anasema ametarajia kupata mtoto kwa takribani miaka 10 bila mafaniko, akiuona umri ukimtupa mkono na hajafanikiwa kuitwa mama na kuamua kutumia fedha yake kwa kiwango chochote kugharamia IVF.

IVF ni mbinu ya kisasa ya kitabibu inayowezesha mfumo wa kuunda mimba kiteknolojia hospitalini, ambayo imekuwa maarufu, nchi za Afrika ikiwamo Tanzania, huku watoto milioni nane wakikadiriwa kuzaliwa kutokana na IVF, kwa mujibu wa European Society of Human Reproduction and Embryology.

Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk. Living Colman, anasema kesi za wenza kushindwa kupata watoto zinaongezeka na kwamba kwenye kliniki kati ya wagonjwa 10 ambao anawaona kila siku hospitalini hapo, watatu wana tatizo hilo, ambalo kitaalamu anataja ni ugumba (infertility).

Kwa takwimu hizo za mtaalamu huyo kutoka MNH, ni kwamba wenye tatizo la ugumba kwa mwezi kutokana na idadi hiyo, huonwa watu 90 na kwa mwaka ikifikia 1,080 wanaohitaji kutibu ugumba.

SIMULIZI YA VENERANDA

Veneranda ni mkazi wa Tabata, jijini Dar es Salaam, ni mjasiriamali ambaye mara baada ya kufanya shughuli zake, muda wa jioni kwa siku tatu za wiki, huutumia kwa kushiriki na waumini wenzake, kanisani kwa ajili ya kusali na shughuli zingine.

Anasali kanisa ambalo halipo mbali sana kutoka nyumbani kwake anakoishi, na ameishi Tabata kwa takribani miaka 20 na ameweza kujenga nyumba yake.

“Ninaishi pekee yangu, sina watoto, mara chache au siku za likizo watoto wa ndugu zangu huja kunitembelea au watoto wa marafiki zangu ambao ninasali nao kanisa moja. Kuna wakati huwa najihisi mpweke, nina bahati mbaya. Wenzangu ambao nina umri au Rika moja, ama nimesoma nao hasa wanawake, wana watoto. Jamii inakutafsiri tofauti, dini nako mtihani,” anasema na kuongeza:

“Kuna wakati siku tulipotoka kwenye ibada ya Jumapili, mmoja wa muumini mwenzangu, mwanaye mwenye umri kama wa miaka nane, tisa, alimuuliza mama yake swali ambalo nilijihisi vibaya, alimwambia...mama tunataenda kwa aunt Veneranda, amesema niende. Mama yake akamjibu utacheza na nani, utamsumbua aunt, mtoto wake akamjibu mama yake…nitacheza na watoto wake!’

Veneranda anasema jibu la mwisho lilimfanya ajisikie vibaya, kisha mazungumzo hayo yalikatishwa baada ya mama wa mtoto kuamua kumuondoa mwanaye kisaikolojia, akimwambia akajumuike na watoto wenzie kucheza, na aache maswali mengi.

“Kwa imani ninakoabudu nafahamu ninachokwenda kukiamua kitanigharimu, kanisa letu kupata mtoto ni majaliwa ya Mungu, na muumini yeyote hutakiwi kutumia njia yeyote mbadala na ukibainika unaweza kuitwa na viongozi wa kanisa au kutengwa. Hivi sasa nimeanza kufanyiwa vipimo na moja ya hospitali binafsi, ili nipandikize mtoto kwa IVF,” anasema Veneranda na kuongeza:

“Na mwanzo wa huduma hii ninatakiwa kukaa ‘bed rest’ (mapumziko) nisifanye kazi ngumu. Kanisani sijaonekana takribani miezi miwili na sijamtaarifu kiongozi yeyote, watakapofahamu, sijui itakuwaje.”

TATIZO LILIKO 

Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi, (MNH), Dk. Colman anasema ugumba ni hali ya mume na mke, kushindwa kupata ujauzito kwa zaidi ya mwaka mmoja, bila ya kutumia uzazi wa mpango wowote.

“Mzizi wa 'infertility' inategemea na chanzo, kwa mwanamke chanzo kikuu ni hormonal cimbalance' (mayai kushindwa kupevuka kwa mpangilio) na hii inaweza kutokana na ‘genetics’ (urithi) lakini pia ulaji mbaya, sukari nyingi na mafuta, husababisha unene uliopitiliza. 

“Pia kupungua sana uzito (anorexia nervosa) inaweza kusababisha ugumba. Mirija kuziba ndio sababu ya pili ya ugumba kwa mwanamke na hii husababishwa na ngono zembe kama nilivyoeleza.

Anasema kwamba, kwa mwanaume sababu ya ugumba inaweza kutokana na  kushindwa kuzalisha mbegu, kutokana na mambo mbalimbali, ikiwamo ulevi wa kupindukia, sigara na pia kuziba kwa virija vya kupitisha mbegu inayosababishwa na maambukizi kama ya PID.

“Tiba ya ugumba ni kumuona mtaalamu wa afya (gynecologist) ambapo atafanya vipimo na kugundua tatizo halafu atatoa tiba husika. Kama ni ‘hormonal imbalance’ atapewa dawa na ushauri. Kama mirija imeziba atashauriwa apandikize (IVF).

“Si kweli kwamba matumizi ya dawa za uzazi wa mpango ndio chanzo cha ugumba. Ikiwa zitatumika kwa maelekezo ya mtaalamu, husaidia kuzuia mimba kwa muda fulani.

“Kuwapa watoto dawa za uzazi wa mpango ni kuwapa uhuru wa kufanya ngono zembe, hali inayosabisha kupata maambukizi kwenye via vya uzazi (PID) hivyo kuathiri mirija ya uzazi na kushindwa kupata ujauzito.

Bingwa huyo wa kinamama, anasema kwenye jamii hasa mijini wengi wanatumia njia uzazi wa mpango wa dharura (emergency contraceptive pills) maarufu P2 akiitaja njia hiyo si sahihi kwa kuwa, ikitumika mara kwa mara inapoteza maana yake.

Bingwa huyo anashauri kwamba, watoto wafundishwe kuepuka ngono za utotoni, ambazo ndio chanzo cha maambukizi kwenye via vya uzazi (PID) na kusababisha kuziba mirija na kushindwa kupata mimba.

HUDUMA YA IVF

Huduma ya IVF, ambayo mahitaji yanaongezeka, tayari MHN imeanza maandalizi na maboresho ya kituo rasmi kwa ajili ya huduma hiyo hospitalini hapo ikiwamo ununuzi wa vifaa.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma MNH, Aminiel Aligaesha akizungumza hivi karibuni, anasema maandalizi ya utoaji huduma ya IVF yanaendelea hospitalini hapo na kwamba yatakapokamilika taarifa itatolewa kwa umma.

Bingwa na Mtaalamu wa kutengeneza Watoto kwa njia ya teknolojia (Embriologist) kutoka Hospitali ya Kairuki Green IVF, George Tryphone, anasema hospitali hiyo imeanza kutoa huduma ya upandikizaji baada ya kubaini mahitaji ni makubwa, na tayari kwa mwaka huu awamu ya kwanza wamehudumiwa wanawake 10 na saba ni wajawazito.

Anasema kati ya hao saba, mmoja ana umri wa miaka 52 sasa ni mjamzito, na kwamba gharama za huduma ya IVF huwa ni kati ya shilingi milioni 10 hadi 17 kutegemeana na ukubwa wa tatizo.

SIKU YA UGUMBA DUNIANI

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Merck Foundation, Seneta Dk. Rasha Kelej, akizungumza kwenye mkutano wa waandishi wa habari kutoka barani Afrika, ikiwamo Tanzania, kwa njia ya mtandao, kuadhimisha mwezi wa kujenga uelewa kuhusu ugumba duniani (World Infertility Awareness Month), anasema asilimia 50 ya tatizo la ugumba, huchangiwa na pande zote mbili.

Anasema mwezi Juni, kila mwaka ni maalumu kwa ajili ya kutoa elimu kwa jamii kuhusu tatizo hilo, ili kuondoa unyanyapaa miongozi mwa jamii, akisema wanawake ambao hukosa watoto na wamo kwenye ndoa, hunyanyaswa na kunyanyapaliwa zaidi na ndugu upande wa mume, hasa mawifi, shemeji na wakwe.

“Tatizo la ugumba hasa Afrika matokeo ya utafaiti yamebaini kwamba asilimia 75 yanachangiwa na tiba isiyo sahihi kwa walioambukizwa magonjwa mbalimbali. Mradi wa ‘More Than a Mother and More Than a Father campaign’ unakuja kutoa elimu na kuondoa unyanyapaa,” anasema Dk. Rasha.

Profesa Uldapo Ashiru, Rais wa Jumuiya ya Kiafrika inayoshughulikia masuala ya  Uzazi (African Reproductive Care Society-ARCS), kutoka nchini Nigeria, anasema ugumba limekuwa tatizo la kidunia, huku takwimu za tatizo hilo zaidi likiongezeka kwenye nchi za Afrika, akitaja sababu mojawapo ni msongo wa mawazo.

“Nimefanya kazi kwa miaka takribani 42, zamani wakinamama walifika kliniki peke yao kuhusu tatizo hili, lakini sasa hata wanaume wana tatizo. Mwanamke akifikisha umri wa miaka 37 na kuendelea vikwazo vya kutopata ujauzito huongezeka. Sasa Nigeria kuna mfumo ambao unamwezesha mwanamke kutunza mayai yake kwenye benki maalum kama ilivyo benki ya damu.

“Mayai hutunzwa kwa muda mrefu, teknolojia hii inasaidia wanawake ambao kwa sasa hawapo tayari kupata mtoto kutokana na shughuli za masomo, kazi au kuchelewa kuolewa. Atakapofikisha umri wowote akishindwa kupata ujauzito atapandikizwa mayai aliyoyatunza benki, hata akiwa na umri wa miaka 50,” anasema bingwa huyo wa kinamama na uzazi.

Rais wa Shirikisho la Muungano wa Vyama vya Uzazi (International Federation Fertility Societies and Gynaecologist), Dk. Edgar Macanu anasema tatizo la ugumba, linajitokeza zaidi kwa wanawake kuanzia umri wa miaka 37  na kuendelea, kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo za kimazingira au kibaolojia.

 

No comments:

Post a Comment

Pages