HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 28, 2023

Watakiwa kuacha kujihusisha na ngono, kuepuka mimba za utotoni

Mbunge wa Vitimaalum Dar es Salaam, Janejelly Ntate (aliyesimama) akizungumza na wadau mbalimbali wa masuala ya wanawake (hawapo pichani) kuhusiana na umuhimu wa watoto wa kike kuacha kujihusisha na ngono katika umri mdogo.


Na Janeth Jovin 


WANAFUNZI wa kike wameshauriwa kuachana na kujihusisha na mapenzi na vitendo vya ngono katika umri mdogo ili kuepuka kupata mimba za utotoni na magonjwa mbalimbali ya zinaa kama vile ukimwi.



Ushauri huo ulitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mbunge wa viti maalumu mkoa wa Dar es Salaam, Janejelly Ntate wakati akifungua majadiliano kuhusu upazaji wa sauti za wanawake katika utekelezaji wa masuala maalum ya uzazi salama, upunguzwaji wa vifo vya uzazi na udhibiti ya ongezeko la mimba za utotoni na zisizohitajika.



Ntate alisema kama wasichana hao hasa waliopo shule za msingi na sekondari watafundishwa kwa kina hasara za kuanza ngono katika umri mdogo kutasaidia kundi hilo kuepukana na mimba hizo za utotoni na magonjwa ya zinaa.



"Tunataka kubadilisha maisha ya vijana wote wa kike na kiume kuondokana na ukatili na mimba hizi za utotoni,  ili tuweze kufanikiwa tunapaswa kuungana kwa pamoja sisi wabunge, taasisi binafsi na waandishi wa habari kupaza sauti zetu na tusiyache mazungumzo kwenye meza. 



"Wakati huu ambao tuna rais mwanamke na baadhi ya wizara vikiongozwa na wanawake ndio muda sahihi wa kukemea kwa sauti moja masuala haya ya mimba za utotoni ambazo zina zima ndoto za mabinti wengi hapa mchini kwetu, " alisema



Aidha alisema anatambua kuwa wakati mwingine vijana wa kike na kiume ujiingiza katika matatizo mbalimbali kutokana na changamoto ya kiuchumi hivyo wakielimisha juu ya mikopo inayotolewa na halmashauri itawasaidia kupata fedha za kuweza kujikimu kimaisha.



"Vijana hawa wa kike na kiume wakiwa na biashara hakuna mtu atakayeweza kuja kuwasumbua, waelimishwe na kupewa miongozo sahihi ya kuweza kupata mikopo hii ya halmashauri, mtoto anapomaiza shule akipata mkopo na kuanzisha biashara inamsaidia kuendelea kutimiza ndoto zao," alisema Ntate



Naye Diwani Kata ya Mbezi Juu jijini Dar es Salaam, Anna Lukindo alisema ni ukweli uliyowazi mfumo wa maadili umeporomoka huku idadi kubwa ya watoto hasa wa kike kuharibikiwa kwa kupata mimba za utotoni ikiongezeka.



Alisema wadau mbalimbali wa masuala ya wanawake na watoto wa kike wanapaswa kuendelea kupiga kelele ili watoto waweze kujikinga na mimba za utotoni.



Naye Mratibu wa Kituo cha Usuluhishi (CRC), Gladness Munuo alisema majadiliano hayo yaliandaliwa na kituo hicho kwa kushirikiana na Shirika la Kiakanda liitwalo Gender Links (GL) lililopo Johanesburg kwa pamoja na Shirika linalotoa Elimu ya Afya ya Uzazi, VVU na Ukimwi (SAfAIDS), lililopo Harare-Zimbabwe.



Munuo alisema wadau waliofika katika majadiliano hayo kwa pamoja walilenga pia kujadili uwepo wa viashiria vyote vinavyoleta vifo vya uzazi vinavyoweza kuzuilika ikiwa ni pamoja na utoaji mimba usio salama kwa kuangalia ‘Sheria za Tanzania’.

No comments:

Post a Comment

Pages