HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 02, 2023

WAOKOTA TAKA BUKOBA KUWEKEWA MAZINGIRA BORA

 

Mkuu wa Kitengo cha usimamizi wa taka na usafi wa mazingira Manispaa ya Bukoba,  Tambuko Joseph.

Bi Lydia Mwaka mmoja ya waokota taka Manispaa ya Bukoba akiwa katika eneo lake la kazi.
 


Na Lydia Lugakila Bukoba

Ikiwa Marchi Mosi ya kila mwaka Dunia huadhimisha siku ya waokota taka Duniani, Waokota taka Manispaa ya Bukoba Mkoani Kagera  wametakiwa kutunza vitendea kazi vyao huku Serikali ikiahidi mikakati mizuri kwao ikiwa ni pamoja na kuendelea kujali afya zao kwa kupimwa kila mara ili kufanya kazi zao bila kupata madhara.

Kauli hiyo imetolewa na Marchi Mosi mwaka huu na Mkuu wa Kitengo cha usimamizi wa taka na usafi wa mazingira Manispaa ya Bukoba   Tambuko Joseph kwa niaba ya Mkurugenzi wa Manispaa hiyo wakati akizungumza na mtandao huu Ofisini kwake.

Amesema kuwa Serikali inatambua mchango wao muhimu katika kusafisha Mazingira huku ikitambua madhara yanayoweza kujitokeza kwa waokota taka kwani zipo taka ngumu zenye madhara kiafya hivyo watahakikisha shughuli hiyo inafanyika kwa umakini huku wakiendelea kuwakinga dhidi ya madhara yanayoweza kujitokeza mara wanapoanza shughuli hiyo hadi kuikamilisha.

Amesema kuwa Manispaa hiyo kwa kushirikiana na wafanya kazi wa Mazingira wamekuwa wakishirikiana  vyema katika kuzoa taka na kuokota taka.

"Taka za kwenye maeneo ya fukwe ya ziwa Victoria huwa tuna utaratibu wa kuziokota hivyo tumeendelea kutambua mchango wao na thamani yao" alisema Tambuko.

Tambuko amesema kuwa wataendelea na zoezi hilo kwa kushirikiana ili mji wa Bukoba iendelee kuwa safi.

Akizungumza malalamiko ya Wananchi juu ya urundikwaji wa taka katika baadhi ya  maeneo amesema taka hizo huwa zina ratiba zake  maalum na kuwataka Wananchi kuendana na ratiba iliyopo ya uondoaji wa taka hizo.

Amewahimiza Wananchi katika Manispaa hiyo kufuata utaratibu uliopo wa kuweka taka katika maeneo wanayoelekezwa  pindi wawapo Barabarani ili kuepuka kuchafua maeneo ya mji huo.

Akizungumzia  upande wa vifaa vya kazi kwa waokota taka amesema kuwa Manispaa imezingatia suala hilo kwa umakini kwani wamekuwa wakiwapatia vifaa vipya kwa ajili ya kujikinga na maradhi kutokana na  kuwepo kwa taka ngumu za aina mbali mbali ambazo nyingine usipokuwa makini unaweza pata maambukizi hivyo wamekuwa wakiwakagua kila wakati kabla ya kushiriki katika shughuli za usafi.

Amesema kuwa kwa sasa wanapambana kuhakikisha wanawabana baadhi ya wafanya kazi katika shughuli hiyo wanaodhaniwa kuuza vifaa hivyo na kuishia kusema vimepotea.

Ameitaja  mikakati waliyonayo kuwa ni kuhakikisha watenda kazi hao wanakuwa na vifaa muhimu huku vingine vinapochakaa wanabadilishiwa ili kulinda afya zao.
 
Ameongeza kuwa kwa kuwajali watenda kazi hao baada ya kupita katika usahili kwanza kabisa wamekuwa wakihakikiwa afya zao kwa mujibu wa Sheria  ya afya ya jamii ya 2009 na Sheria nyinginezo na kupimwa afya kila baada ya miezi 6 ili wafanye kazi hiyo wakiwa na afya nzuri na imara.

Ametoa wito kwa Wananchi Manispaa ya Bukoba kutumia vyombo vilivyowekwa Barabara ili kutunza Mazingira huku akizisitiza kuwa shughuli ya usafi ni shirikishi kwa Kila mtu hivyo waheshimu siku maalum za usafi ambazo ni siku ya  Alhamisi ya kila wiki na Jumamosi ya mwisho wa kila mwezi ikiwa ni pamoja  kuchangia ada ya taka.

Hata hivyo kwa upande wake Muokota taka Manispaa ya Bukoba  Bi Lydia Miaka amewaomba Wananchi  kutodharau kazi yao na kuacha tabia ya kutupa taka ovyo huku akiiomba Serikali kuboreshea zaidi  mazingira yao ya Kazi.

No comments:

Post a Comment

Pages