HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 21, 2013

SERIKALI MKOANI SHINYANGA YAONDOA BAADHI YA MICHANGO INAYOWAELEMEA WAZAZI

Serikali Mkoa Shinyanga imeondoa baadhi ya michango inayotozwa katika shule za Sekondari ambayo imekuwa kero na mzigo kwa wazazi, hasa mwanafunzi anapoanza kidato cha kwanza.

Maamuzi hayo yamefikiwa katika kikao cha Wadau wa Elimu kilichofanyika jana chini ya Mwenyekiti wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mheshimiwa Ally Nasoro Rufunga ambacho kiliwahusisha wadau mbalimbali wa Elimu ndani ya Mkoa kuanzia wanafunzi, wazazi, walimu,viongozi wa serikali,wataalamu wa Elimu na viongozi wa vyama vya siasa,asasi za serikali na binafsi.

Michango hiyo imeondolewa baada ya wazazi wengi kutoa malalamiko kwa Mkuu wa Mkoa kuwa, kumekuwa na michango mingi mbali na karo, ambayo wazazi wanashindwa kumudu gharama hivyo kushindwa kupeleka watoto wao shule kwa wakati kwa sababu wazazi wengi wana kipato cha chini.

Michango iliyoondolewa ni pamoja na michango ya Majengo, masweta na sare za shule.

Mkuu wa Mkoa alikieleza kikao kuwa, pamoja na maamuzi hayo, serikali itapeleka maelekezo katika bodi na kamati za shule ziwasilishe Mkoani aina yoyote ya michango iliyokubalika katika vikao vya bodi na kamati hizo ili Mkoa uidhinishe michango hiyo kama ina umuhimu.

Aidha,katika kikao hicho serikali ya mkoa wa Shinyanga imeazimia kuboresha Elimu katika mkoa huu kwa kuanza kufanyia kazi baadhi ya changamoto na kisha kufanya tathmini baada ya mwaka mmoja kwa lengo la kumaliza tatizo moja baada ya lingine.

Changamoto zilizopewa kipaumbele ni Kuhakikisha wanafunzi wanapata chakula shuleni, kuongeza idadi ya walimu hasa maeneo ya vijijini na kuimarisha idara ya ukaguzi wa shule, pia, kukamilisha idadi ya madawati ya kutosha, kuthibiti utoro na mimba kwa kuwachukulia hatua kali za kisheria wanaosababisha utoro kwa wanafunzi na wanaowapa mimba pamoja na kuongeza motisha kwa walimu waajiriwa wapya wanaoripoti.

Mkuu wa Mkoa pia amewazawadia wanafunzi waliofanya vizuri katika ngazi ya mkoa katika mitihani ya Mwaka jana 2012 darasa la saba, kidato cha nne na kidato cha sita pamoja walimu wao waliofanyan vizuri.

Akifunga kikao hicho amewataka wadau wote kusimamia sheria zilizopo kwa kila mmoja kuwajibika katika sehemu yake, hususani Maafisa Elimu wa Wilaya amewataka wasifanye kazi kwa mazoea.

No comments:

Post a Comment

Pages