NA JOHN
MARWA
TAASISI ya Network for Vulnerable Rescue Foundation (NVRF
Sports Academy), wakishirikiana na Right to Play, wamezikosha nyoyo za wakazi
wa mtaa wa Kigogo jijini Dar es Salaam kwa tamasha la uhamasishaji wa haki za
watoto, vijana na wanawake katika jamii.
Tamasha hilo lilifanyika juzi kwenye viwanja vya Musako mtaa
wa Kigogo Kati, ambako michezo mbalimbali ilifanyika.
Miongoni mwa michezo iliyofanyika ni Soka, Maigizo yenye
kufundisha stadi za maisha na kutoa fursa ya kuwalinda watoto wa kike na
vitendo viovu, na elimu ya jinsia kwa vijana.
Akizungumzia tamasha hilo, Meneja Mipango wa Right to Play
Tanzania ambao ni washirika wa NVRF, Maria Mongi, alisema jamii isikate tamaa
katika harakati za kuwakomboa watoto, vijana na wanawake kwenye changamoto
zinazowakabili kila uchao.
“Pia kama Right to Play, tunafurahishwa na kazi nzuri
inayofanywa na NVRF katika kukwamua vikwazo mbalimbali vinavyoikumba jamii kwa
kutoa elimu ya kujitambua na kijinsia kwa vijana na wanawake, huku wakiongeza
hamasa ya haki ya mtoto kupata elimu,” alisema.
Mongi, alisema wanajivunia kuona ufadhili wanaoutoa kwa NVRF
unatumika vizuri licha ya kuwa hautoshelezi, lakini wanaonyesha nia ya dhati ya
kuisaidia jamii.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa NVRF Sports Academy, Peter
Mwangi, alisema amefurahishwa na uwepo wa washirika wao, kwani unawaongezea
hamasa ya kuendeleza harakati za ukombozi kwa mtoto, kijana na mwanamke kupitia
michezo.




No comments:
Post a Comment