HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 01, 2019

Tanzania kete ya mwisho Doha Qatar

Ofisa Michezo wa Jiji la Arusha, Benson Maneno (kulia), akimkabidhi bendera ya Taifa nahodha wa timu ya Taifa ya Riadha inayokwenda kushiriki mashindano ya Dunia Doha Qatar, Alphonce Simbu. Hafla hiyo ilifanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha. (Na Mpiga Picha Wetu). 

NA MWANDISHI WETU

WANARIADHA watatu wa Tanzania waliosalia kwa ajili ya mashindano ya Dunia ‘IAAF World Championships’, wanatarajiwa kuondoka nchini kesho (Oktoba 2) kwenda Doha, Qatar kwa ajili ya kinyang’anyiro hicho.

Timu ya Tanzania kwa ajili ya mashindano hayo ilikuwa na Wachezaji wanne, ambako mmoja Failuna Matanga, tayari amekwishashiriki katika Marathon Septemba 27 mwaka huu na kushindwa kumaliza, akijitoa katika Kilomita 21.

Kwa sasa matumaini ya Watanzania yako kwa Mshindi wa Medali ya Shaba katika mashindano yaliyopita huko London, Alphonce Simbu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Agustino Sulle kutoka Klabu ya Talent na Stephano Huche wa African Ambassador Athletics Club (AAAC), wakiongozana na Kocha Andrew Panga, ambao wanaondoka leo wakipitia Nairobi, Kenya.
Wanariadha hao wote, watakimbia Marathon ‘Kilomita 42.195’ Oktoba 5 mwaka huu.

Kwa upande wake, Nahodha wa timu hiyo, Alphonce Simbu, alisema ingawa kila mmoja kajiandaa katika mazingira magumu, lakini wanakwenda kupambana kuipigania nchi yao.

“Tahadhari ya hali ya hewa ya huko wote tumeipata, tutakwenda kupambana na naamini tutafanya vizuri, kikubwa tunaomba Watanzania watuombee tu,” alisema.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday, ambaye yuko Doha Qatar, maandalizi ya timu hiyo kupokelewa na itakapofikia yako tayari.

Gidabuday, alisema pia Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Fatuma Mohamed Rajab, amewaandalia hafla ya chakula wachezaji hao Oktoba 4 kabla ya kuingia kibaruani Oktoba 5.

No comments:

Post a Comment

Pages