HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 28, 2019

JAMII YATAKIWA KUTOFUMBIA MACHO VITENDO VYA UKATILI KWA WANAWAKE

Na Tatu Mohamed
JAMII imetakiwa kutokuvifumbia macho vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto kwani ni kinyume na haki za binadamu. 

Wito huo ulitolewa jijini Dar es Salaam na Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu, Nyanda Shughuli katika maadhimisho ya Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia yaliyoandaliwa na TGNP mtandao yenye kauli mbiu ya 'Kizazi cha Usawa, Simama dhidi ya Ubakaji'.

Alisema ni vyema suala la ukatili wa kijinsia likatazamwa kwa jicho la tofauti, kwani bado kuna kazi kubwa katika jamii ya kubadili mtazamo pamoja na fikra. 

"Nitoe wito kwa jamii isivifumbie macho vitendo hivi, vinaumiza sana na ni kinyume na haki za binadamu. Mnapokutana na matukio mbalimbali ya aina hii mshirikiane na vyombo husika, hii itawezesha kuwachukulia hatua wanaoendeleza vitendo hivi," alisema Shuli. 

Aliongeza kuwa tume itaendelea kuelimisha jamii ili kuhakikisha wanawake na haki za watoto zinazingatiwa. 

"Taifa lisilo na ukatili wa kijinsia ni taifa lenye maendeleo ya kasi. Tulitazame suala hili kwa jicho la tofauti. Tuendelee kushikamana kuhakikisha kila mmoja katika nafasi yake anapambana kuvitokomeza," alisema Nyanda. 

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao, Lilian Liundi, alisema ukatili dhidi ya wanawake unaathari kubwa si tu kwa wanawake bali pia katika uchumi wa nchi na maendeleo pamoja na ustawi wa jamii kwa ujumla. 

"Tanzania ya Viwanda Wanawake ni Msingi wa mabadiliko ya kiuchumi. Tunpozungumzia Tanzania ya viwanda wakati wanawake zaidi ya asilimia 30 wanaendelea kufanyiwa ukatili wa kijinsia hivyo hawawezi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi ni changamoto kubwa sana.

"Mimi naamini kuwa kukiwa na mgawanyo mzuri wenye usawa, wanawake na wasichana wataweza kufikia fursa za kiuchumi na maarifa itawasaidia kufanya maamuzi mazuri katika familia na jamii na kuongeza kasi ya maendeleo," alisema. 

Aidha alisema tunapoelekea kuadhimisha miaka 25 ya Ulingo wa Beijing, pia tunapaswa kutafakari kwa kina hatua iliyopigwa katika kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia na kuweka mikakati itakayowezesha kukomesha kabisa ili kuweza kufikia maendeleo endelevu.

No comments:

Post a Comment

Pages