HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 12, 2020

POLISI WAWAKWAZA MADIWANI-SIKONGE

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge Martha Luleka akitoa ufafanuzi kwa Madiwani kwenye mkutano wa Baraza la Madiwani la Sikonge la kujadili na kupitia mapendekezo ya makisio ya mapato na matumizi ya mwaka 2020/21.


Na Mwandishi Wetu

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge wameiomba Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora kuchunguza nia ya Polisi kutoka Mkoani kwenda katika Kijiji cha Mpombwe na kuanza kuchukua bidhaa kwenye maduka bila Kamati ya Usalama ya wilaya Sikonge kuwa na taarifa.
Ombi hilo la Madiwani lilitolewa jana baada ya Diwani wa Kata ya Mpombwe Juma Mdulla kueleza tukio lilitokea tarehe 8 Januari mwaka huu katika Kijiji hicho wakati akichangia hoja kwenye  mkutano wa Baraza la Madiwani la Sikonge la kujadili na kupitia mapendekezo ya makisio ya mapato na matumizi ya mwaka 2020/21.
Alisema Polisi kutoka Tabora mjini walifika katika Kijiji hicho na kwenda kwa Mwenyekiti wa Kijiji kumtaka awaongoze kuendesha ukaguzi bidhaa zilizokwisha muda wake kwenye maduka yalipo eneo hilo.
Diwani huyo alisema kuwa cha kusikitisha walifanya kazi hiyo wakiwa pekee yao bila hata kuwa na wataalamu wa Shirika la Viwango Tanzania na viongozi wengine kama Wataalamu wa sekta ya Afya na Mtendaji wa Kata.
Aliongeza kuwa katika ukaguzi huyo walichukua baadhi ya vipodozi na mafuta ya Petroli jambo ambalo liliacha maswali mengi.
Mdulla alisema kuwa alipojaribu kufuatilia juu ya taarifa za uwepo wa zoezi hilo hakupata majibu alibaini kuwa polisi hao walifika na kuanza kazi bila hata kutoa taarifa katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Sikonge na wala hawakusaini Kitabu cha Wageni cha Kijiji hicho, jambo ambalo limeacha maswali kama kweli Polisi hao walikuwa kazini au walikuwa katika shughuli zisizo halali.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge Peter Nzalalila alisema kitendo kilichofanywa na Polisi hata kama kilikuwa halali walipaswa watoe taarifa katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya na kuongeza kuwa vema Mkuu wa Mkoa wa Katibu Tawala Mkoa wakapelekewa taarifa hiyo ambayo imewasikitisha.
Alisema kumezuka tabia ya Taasisi mbalimbali kuingia katika Wilaya ya Sikonge na kuendesha shughuli zao na wakati mwingine kuwabughuzi wananchi bila hata kutoa taarifa kwa Mamlaka ya Juu za Wilaya ikiwemo kwa Kamati ya Usalama ya Wilaya.
Kwa upande wa Katibu Tawala Wilaya ya Sikonge Renatus Mahimbali alisema utaratibu unataka kabla ya Taasisi yoyote haijaanza kazi yake ni vema ionyeshe vibali vinavyowataka kufanyakazi hiyo na watoe taarifa katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya.
Alisema watu wanaoingia Sikonge na kuendesha shughuli zao bila Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kuwa na taarifa watachukuliwa kama waharifu.
Katibu Tawala huyo wa Wilaya ya Sikonge alitoa mfano hivi karibuni alipata taarifa kutoka kwa wananchi ya kuwepo na watu wanaodai kuandikisha wastaafu na alipojaribu kuwahoji kwa njia ya simu na walipobaini kuwa utapeli wao umegundulika walikata simu na kuondoka.
Aliwaomba Madiwani kuhakikisha kuwa wanapoona wageni wanaendesha shughuli katika maeneo yao wawaombe vibali vinavyowapa ruhusa ya kufanyakazi hiyo.

No comments:

Post a Comment

Pages