HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 08, 2020

Raia Wawili wa Kenya na Watanzania kizimbani kwa kudaiwa kuisababishia hasara TCRA kiasi cha Milioni 16.6

 

Na Janeth Jovin

RAIA wawili wa Kenya na Watanzania  wawili,  wamefikishwa  katika  Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka ya uhujumu uchumi ikiwemo kuisababisha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hasara ya Sh milioni 16.6.

Washitakiwa hao ni Beth Ngunyi (43) mfanyabiashara  na Mkazi wa Kasaram Nairobi, Frolence Dirango (34)  mfanyakazi wa Kampuni  ya Betlee  kama Ofisa wa Teknolojia ya Habari  na Mawasiliano, Alven Swai (26) mkazi wa Mbezi Beach na Godluck  Macha (28) mfanyabiashara  na Mkazi wa Mbezi beach.

Akisoma hati ya mashtaka mahakamani hapo leo, Wakili wa Serikali, Batilda Mushi amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu,  Yusto Ruboroga  kuwa kati ya Julai  Mosi na Julai 26, mwaka huu katika  maeneo mbalimbali, washtakiwa  kwa pamoja  walikula njama ya kutumia vifaa vya mawasiliano.

Amedai Julai 13, mwaka huu maeneo ya Tarakea wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro,  Ngunyi na Dirangu waliingiza vifaa vya kielekroniki nchini pasipo kuwa na leseni ya TCRA.

Mushi amedai Julai 20, mwaka huu maeneo ya Kibona Lodge Mbezi Beach jijini  Dar es Salaam, washtakiwa hao walisimika  vifaa vya mawasiliano bila kuwa na leseni  kutoka TCRA.

Katika shtaka la nne, imedaiwa kati ya Julai 20 na 26, mwaka huu maeneo ya Kibona lodge Mbezi beach, kinyume  na sheria walifanyia marekebisho  ya vifaa hivyo vya kielektroniki.

Pia imedaiwa kinyume na sheria washtakiwa  hao waliendesha mitambo ya mawasiliano bila kuwa na leseni kutoka TCRA.

Aidha Mushi amedai kinyume na sheria washtakiwa hao walitumia vifaa vya mawasiliano vilivyounganishwa na vifaa vingine vya mawasiliano kwa nia ya kupokea na kusambaza mawasiliano bila kupata uthibitisho wa TCRA.

Washtakiwa hao wanadaiwa walikwepa kufanya malipo ambayo yalipaswa kufanyika kwa kuruhusu mawasiliano nje ya nchi kutokana na kutumia kifaa hicho cha mawasiliano bila kuwa na leseni.

Katika shtaka  la tisa, imedaiwa Julai 13, mwaka huu maeneo ya Kibona Lodge, Mbezi beach,  washitakiwa Ngunyi na Dirangu wanadaiwa kuwepo nchini bila kuwa na kibali.

Mshtakiwa  Macha amedaiwa Julai 15, mwaka huu  kinyume  na sheria aliwahifadhi Ngunyi na Dirangu kuishi kwenye Jamhuri ya Muungano  wa Tanzania  wakati wakijua hawana kibali.

Katika shtaka la 11, imedaiwa kati ya Julai 20 na 26, mwaka huu maeneo ya Kibona lodge Mbezi beach jijini Dar es Salaam  washitakiwa  hao waliisababishia TCRA hasara ya Sh 16,634,400.

Washtakiwa  hao hawakutakiwa kujibu chochote  kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu  uchumi.

Upande wa mashtaka  ulidai upelelezi  wa kesi hiyo bado haujakamilika  na kuomba tarehe nyingine  kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Ruboroga  aliahirisha  kesi hiyo  hadi Agosti  20 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa na washtakiwa  wote  wamerudishwa rumande  kwa sababu mashitaka  hayo hayana dhamana labda watakapoomba Mahakama Kuu.

No comments:

Post a Comment

Pages