Afisa Masoko wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar Khalfan Ali Mohamed wa Kwanza (kulia), akimsikiliza mteja hivi karibuni ndani ya banda lao katika Maonyesho ya 45 ya Kimataifa ya Biashara Dar és Salam maarufu (Saba Saba).
Na Asha Mwakyonde, Dar es Salaam
AFISA Masoko wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar Khalfan Ali Mohamed amesema kipindi cha miaka mitatu iliyopita kabla ya mlipuko wa virusi vya COVID 19 walikuwa wakipokea wageni kutoka 300,000 hadi kufikia zaidi ya 500,000 kwa mwaka.
Kamisheni ya Utalii Zanzibar ni taasisi ambayo ipo chini ya Wizara na Utalii wa mambo ya kale na Idara ya serikali kazi yake kubwa ni kutangaza Utalii.
Hayo ameyasema hivi karibuni ndani ya banda lao katika Maonyesho ya 45 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salam maarufu (Saba Saba), yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere ambayo yalianza rasmi Juni 28 na kumalizika Julai 13 mwaka huu amesema idadi hiyo inaonyesha ni kiwango kizuri kwa sekta ya Utalii na ilionyesha matokeo chanya.
Afisa huyo amesema idadi hiyo ya wageni 500,000 inatokana na sera na mpango mkakati wa Utalii wa Zanzibar kufikia mwaka 2020 na kwamba mwaka 2018 tayari walishafikia malengo.
Amesema serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka jitihada za kukuza Utalii na kwamba virusi vya COVID 19 uliathiri sekta ya Utalii sio kwa Zanzibar tu bali duniani kote.
" Zanzibar pia iliathirika kwa kua nchi nyingi zilifunga mipaka yake ikawa ni ngumu Wakala wa Utalii kuleta wageni,. Tuliathirika kidogo Februari hadi Mei mwaka 2020 hali haikuwa nzuri "amesema.
Ameongeza kuwa kuanzia Julai baadhi ya mataifa yalifungua mipaka yake na kwamba mwaka huu wanatarajia kupata matokeo chanya.
Afisa Masoko huyo ameeleza kuwa wanaendelea kutangaza sekta ya Utalii kwa nguvu na jitihada zote na kwa sasa serikali hiyo imejikita kuwekeza katika vivutio vilivyopo baharini.
" Uchumi wa bluu unaendana na sekta ya Utalii na tutegemee wageni wengi kufika Zanzibar. Tupo hapa katika Maonyesho haya kuhakikisha tunatoa elimu na kuwafahamisha Watanzania kuja kutembelea vivutio vilivyopo Zanzibar," amesema.
Ameongeza kuwa serikali ya awamu ya nane kupitia Rais Dkt. Hussein Ally Mwinyi inahamasisha Utalii na uchumi wa bluu na kuwataka wananchi kwenda Zanzibar kutembelea vivutio vilivyopo sehemu za fukwe.
Amesema Zanzibar inasifika kwa muda mrefu kuwa ina vivutio vya utamaduni asili na watu wake wakarimu, manzari mazuri na fukwe mwanana.



No comments:
Post a Comment