HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 03, 2021

Waziri Jafo: NMB mnaitendea haki Tanzania na watu wake

 


Mkuu wa Kitengo cha Biashara za Serikali Vicky Bishubo, akiaangalia Meza na viti kabla ya kumkabidhi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Suleiman Jaffo kwa ajili ya Shule ya Sekondari Mzenga, Kushoto ni Kaimu Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Mashariki, Harold Lambileki. 


 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazimngira, Suleiman Jaffo, akipongezwa na Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mzenga baada ya kupokea Meza na viti vilivyotolewa na Benki ya NMB wakati wa hafla iliyofanyika Kisarawe jana. Katika ni Mkuu wakitengo cha Biashara za Serikali Vicky Bishubo  Kushoto ni Meneja wa NMB tawi la Kisarawe, Justina Kikuli. Benki ya NMB kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii ( CSR) ilikabidhi madawati na mabati kwa shule ya ya Msingi Chanzige A na ya Sekondari Mzenga zote zikiwa wilayani kisarawe.  



Mkuu wa Idara ya  Biashara za Serikali  wa NMB ,Vicky Bishubo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Sulemani Jafo, Kaimu Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Mashariki, Harold Lambileki, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Chanzige A pamoja na wanafunzi wakiwa wameshika moja ya bati zilizokabidhiwa kwa shule ya Msingi Chanzige A iliyopo wilayani Kisarawe mkoa Pwani.




NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira, Seleman Jafo, ameitaja Benki ya NMB kuwa ni Taasisi inayoitendea haki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na watu wake kupitia Program ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) na ukubwa wa gawio la benki hiyo kwa Serikali linalotokana na hisa zake.

Waziri Jafo ameyasema hayo Ijumaa ya Julai 30, wakati akipokea msaada wa viti 50, meza 50 na mabati 165, vyote vikiwa na thamani ya Sh. Mil. 10, vilivyotolewa na NMB kwa ajili ya Shule ya Sekondari Mzenga na Shule ya Msingi Chanzige A, zilizoko wilayani Kisarawe mkoani Pwani.

Kauli ya Waziri Jafo, inakuja huku NMB ikiwa imetumia zaidi ya Sh. Bilioni 1.1, kusaidia utatuzi changamoto mbalimbali kwenye Sekta za Elimu na Afya kuanzia Januari hadi Julai 2021, kati ya Sh. Bil. 2 ambazo ni asilimia 1 ya faida yake ya mwaka uliopita, ambazo zinatumika kutoa misaada mwaka huu, ambao pia imekabidhi serikalini gawio la Sh. Bilioni 21.76.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Viwanja vya Shule ya Msingi Chanzige A, mjini Kisarawe, Waziri Jafo alisema ukubwa wa kiasi cha Sh. Bil. 2 ilizotenga NMB kusaidia nyanja za Elimu na Afya, unathibitisha namna benki hiyo inavyoiishi kaulimbiu yao ya Karibu Yako.

"Kiasi hicho kinaenda kuunga mkono jitihada za Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kutatua kero mbalimbali katika elimu na afya, nyanja ambazo zinanufaika pia na Mipango ya Maendeleo ya Serikali kupitia bajeti zake, zinazopewa nguvu pia na ukubwa wa gawio la NMB kutokana na hisa zetu kwao.

"Kwa dhati, niseme NMB mnaitendea haki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na watu wake, kwani hamjawahi kuwa nyuma katika kuisapoti Serikali kutatua kero za jamii, hii inawafanya Watanzania kujivunia uwepo wenu. Tuliziomba taasisi nyingi, Ila nyie mkawa wa kwanza kutujibu na leo kutukabidhi misaada hii," alisema.

Waziri Jafo, ambaye pia ni Mbunge wa Kisarawe, aliipongeza NMB kwa kazi kubwa inayofanya kila uchao wilayani humo, huku akiiomba kuendelee kusaidia, sambamba na kuangalia uwezekano wa kujenga tawi dogo la benki hiyo huko Maneromango, ili kuwaondolea wananchi na watumishi wa umma adha ya kutembea na pesa kufuata huduma za kibenki mjini Kisarawe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitenho cha Biashara za Serikali wa NMB, Vicky Bishubo, alimhakikishia Waziri Jafo kuwa changamoto za Sekta ya Elimu na Afya ni kipaumbele cha benki yake, kutokana na ukweli kuwa elimu na afya ndio ufunguo, msingi na mtaji mkuu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

"NMB tunatambua juhudi za Serikali kusimamia elimu na afya kwa nguvu zote kwa kuboresha mazingira ya utoaji huduma hizo mijini na vijijini, na tunaipongeza. Pamoja na jitihada hizo, sisi kama wadau, tunajiona tunao wajibu wa kuunga mkono kuikwamua jamii, ambayo inatufanya NMB kuwa benki kubwa na bora kuliko zote nchini," alisema Bishubo katika hafla hiyo.

Naye Kaimu Meneja wa NMB Kanda ya Mashariki, Harold Lambileki, aliishukuru Serikali wilayani Kisarawe kwa ushirikiano inaouonesha kwa benki yake na kuahidi kuudumisha kwa maendeleo endelevu ya Kisarawe, huku Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Mwanana Msumi, aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya, akisema inatambua na kuthamini mchango wa NMB kwa ustawi wa wilaya na wananchi wake.

No comments:

Post a Comment

Pages