HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 27, 2022

Siku ya Uzazi wa Mpango

Na Irene Mark

WAKATI Dunia ikiadhimisha siku ya uzazi wa mpango kila Septemba 26 ya mwaka, suala la utoaji mimba kwa njia zisizo salama linachangia ongezeko la vifo vitokanavyo na uzazi.

Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFA), inaeleza kuwa vifo vya uzazi nchini Tanzania viliongezeka hadi vifo 556 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2015 kutoka vifo 454 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2010.

Daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake na uzazi, Elias Kweyamba anasema asilimia kati ya 16 hadi 19 ya vifo vya uzazi vinatokana na utoaji wa mimba usio salama.

Kwa sababu hiyo ipo haja ya Dunia husasani kwa nchi zinazoendelea kupata elimu sahihi ya njia za uzazi salama ili kuepuka mimba zisizotarajiwa ambazo mara nyingi hutolewa kwa njia hatarishi.

Wakizungumza na HabariMseto Blog kwa nyakati tofauti baadhi ya wanawake waliofika kwenye Zahanati ya Mpunguzi jijini Dodoma kupata huduma za kliniki pamoja na watoto wao wamesema elimu zaidi inahitajika hasa kwenye matumizi ya njia za uzazi wa mpango.

Wameeleza namna wanavyokosa elimu ya kupambana na maudhi madogomdogo baada ya kutumia njia za kupanga uzazi hali inayowalazimu kusitisha matumizi ya njia hizo na kuwasababishia kupata watoto wasiowatarajia na kutoa mimba kwa njia hatarishi.

Wanawake hao pia hawana taarifa za uwepo wa siku ya kupanga uzazi duniani ambayo kimsingi inawahusu katika kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi lakini pia kuwa na afya njema huku wakishiriki kazi za kiuchumi kwa maslahi ya familia zao na taifa.

Katika kuadhimisha siku hiyo kila mwaka serikali, mashirika kibinafsi, vyombo vya habari na watu mbalimbali hukusanyika na kujadili masuala muhimu ya upatikanaji wa huduma bora za uzazi wa mpango.

Tafiti mbalimbali za wana taaluma chini ya UNFPA zinaonesha kwamba zaidiee ya wanawake na wasichana bilioni 1.8 wako katika kundi la umri wa uzazi lakini wengi wao wanakabiliwa na vikwazo ambavyo ni ukosefu wa taarifa sahihi na huduma bora za kupanga uzazi kutoka kwa watumishi wenye utaalam.

Nchini Tanzania asilimia 32 tu ya wanawake walio katika umri wa uzazi wanatumia njia za kisasa za uzazi wa mpango huku asilimia 22 wakiwa na mahitaji ambayo hayajafikiwa.

Kwa kuzingatia kanuni zilizopo zinazowaweka wasichana kwenye ngono na ndoa za utotoni, asilimia 27 ya wasichana wenye umri kati ya miaka 19 na 15 ni wajawazito au wameanza kuzaa.

Matokeo yake, wanakabiliwa na hatari kubwa za kuharibika kwa mimba, utoaji mimba usio salama, aina nyingine za magonjwa ya uzazi ikiwemo saratani na vifo kutokana na matatizo ya ujauzito na uzazi.

Mbali na hayo, wanawake na wasichana wanashindwa  kutimiza ndoto zao za maendeleo na kukabiliwa na kutengwa katika kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na vyombo vya maamuzi kwa sababu ya kushindwa kusimamia uzazi wao.

Huduma za kupanga uzazi ni moja ya afua mtambuka zinazopewa kipaumbele hasa katika huduma za kinga za afya. Huduma hizo za ni  muhimu katika kufikia malengo makuu ya afya hasa katika afya ya uzazi na Mtoto. Inachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vya uzazi kwa takriban 44% Na kupunguza vifo vya watoto. Huduma hizo ni muhimu katika ukuaji wa uchumi, umaskini na kupunguza njaa, kupambana na VVU/UKIMWI, kukuza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake, kuhakikisha uendelevu wa mazingira, na kukuza secu.

No comments:

Post a Comment

Pages